Na Mwandishi Wetu, JamhuriMedia

Mfuko wa Abbott wenye makao yake makuu nchini Marekani umeahidi kuendelea kushirikiana na Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) katika maeneo mbalimbali ikiwemo kuwajengea uwezo watalaam wa vifaa tiba na baadhi ya kada zenye uhaba zitakazoainishwa hapo baadaye.

Hayo yamesemwa leo na Rais wa Mfuko wa Abbott Bi. Melissa Brotz ambaye yupo nchini kwa ziara ya kikazi ya kutembelea miradi inayofadhiliwa na mfuko huo.

Mfuko wa Abbott uliisaidia MNH kujenga Jengo la Wagonjwa wa Nje (OPD) ambalo huona wagonjwa kati ya 800 hadi 1,000 kwa siku, ulikarabati Maabara Kuu na kutoa msaada wa vifaa vyake kadhaa, ulijenga upya Idara ya Magonjwa ya Tiba ya Dharura (EMD) ambayo kwa sasa inaona wagonjwa 250 hadi 300 kwa siku, umefadhili mafunzo mbalimbali kwa watalaam kada ya afya hususani EMD, utafiti, ubora wa huduma, mifumo ya Tehama n.k.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa MNH Prof. Mohamed Janabi ameupongeza Mfuko wa Abbott kwa ushirikiano na mchango wake mkubwa kwa hospitali.

“Abbott mmefanya kazi kubwa hapa, na kubwa zaidi ni pale ambapo mmesaidia kujenga uwezo wa watalaam kwani ni nyezo muhimu yenye kutuwezesha kuendelea kutoa huduma kwa mfumo endelevu kwa ukishakuwa na utalaam hauharibiki kama vifaa” amesema Prof. Janabi.

Ameongeza kuwa ataendeleza ushirikiano huo kwenda hatua nyingine zaidi ili kuimarisha huduma, uendelevu wa mchango wao kwa hospitali kwa manufaa ya wananchi.

By Jamhuri