ACT-Wazalendo yaitaka Serikali kupitia upya mfumo wa taasisi za mikopo

Na Mwandishi Wetu,JamhuriMedia,Tanga

Makamu Mwenyekiti wa Chama cha ACT Wazalendo Tanzania Bara Dorothy Samu ameitaka Serikali kupitia upya mfumo mzima wa Taasisi zisizo za Kiserikali zinazotoa mikopo na kuangalia riba zao kutokana na kuwa zimekuwa mzigo kwa wanawake na kupelekea kushindwa kurejesha na wakati mwengine kukimbia familia zao

Dorothy ambaye pia ni Waziri Mkuu Kivuli aliyasema hayo leo wakati wa Kongamano la Kitaifa la Wanawake wa ACT lililofanyika Jijini Tanga ambapo amesema mikopo hiyo badala ya kuwa mkombozi kwa wanawake imekuwa mizigo kwao.

Waziri Kivuli wa Wizara ya Wanawake,Watoto na Makundi Maalumu Janeth Rite akizungumza wakati wa kongamano hilo

Amesema kwa lazima Serikali iangalie kwa umakini riba ambazo zimetolewa na taasisi hizo ambayo sio himilivu na sio rafiki kwa wanawake ambao ndio wakopaji wakubwa katika kuendeleza biashara zao za ujasiriamali.

“Katika hili tunaitaka Serikali kuangalia kwa umakini taasisi za mikopo ambazo zimekuwa riba kubwa na kupelekea kushindwa kurejesha na kukimbia familia zao hili ni tatizo liangalie hasa ile inayoitwa Kausha Damu “ amesema.

Awali akizungumza Waziri Kivuli wa Wizara ya Wanawake, Watoto na Makundi Maalumu Janeth Rite aliitaka Serikali kuhakikisha Halamshaueri zinakuwa na uwiono sawa katika utoaji wa fedha za mikopo asilimia 10 zinazotokana na mapato ya ndani.

Amesema kwa sababu hali ilivyo hivi sasa imekuwa ikiwabagua baadhi ya wananachi kutokana na itikadi ya vyama vyao jambo ambalo sio nzuri kwa ustawi wa maendeleo hapa nchini.

“Suala hilo la mikopo zinazotoka kwenye Halmashauri lazima kuwepo na usawa pamoja na kuondosha upendeleo ambao umekuwa ukipelekea manunguniko kwa wanawake kutokana na itikadi zao za kiasiasa” amesema.

Waziri huyo amesema kwamba kwa mujibu wa takwimu zilizopo ni asilimia 80 ya wanawake wapo kwenye sekta ya kilimo ambao wanalima kwa kutumia jembe kilimo ambacho hakina tija kwao kutokana na kupata mazao hafifu.

Amesema kwa sababu hakina tija ndio maana Chama hicho katika mipango tyao watakapo pata ridhaa ya kuongoza nchi watawaondoa kwenye ujasiriamali usiokuwa na tija ikiwemo kuwapeleka wenye tija ambao wanaweza kukopesheka.

“Lakini pia Serikali iweze kuona namna nzuri ya kutoa mikopo kwa wakina mama ili waweze kuongeza wigo mpana wa uzalishaji mazao ya chakula ndipo itapoondosha changamoto zao za kiuchumi “ amesema.

Hata hivyo amesema wakina mama wakiendelea kutumia jemnbe la mkono wasahau mafanikio yao kupitia sekta ya kilimo kutokana na kwamba kuna haja ya kubadilika kwa kulima kisasa.

Makamu Mwenyekiti wa Chama cha ACT Wazalendo Tanzania Bara Dorothy Samu ambaye pia ni Waziri Mkuu Kivuli akizungumza leo wakati wa Kongamano la Kitaifa la Wanawake wa ACT lililofanyika Jijini Tanga ambapo alisema mikopo hiyo badala ya kuwa mkombozi kwa wanawake imekuwa mizigo kwao.