Na Mwandishi Wetu, JAMHURI MEDIA, Dar es Salaam.

Kampuni ya Bima ya Assemble Insurance (T) Ltd imetoa msaada wa luninga 10 kwa Hospitali ya Taifa Muhimbili ikiwa ni sehemu ya mpango wa kampuni hiyo kurejesha kwa jamii.

Akipokea msaada huo Mkurugenzi Mtendaji wa Hospitali ya Taifa Muhimbili, Prof. Mohamed Janabi amesema kuwa msaada huo ni wa manufaa sana kwa MNH kwa kuwa pesa ambazo zingetumika kununulia luninga hizo zitaelekezwa kwenye mahitaji mengine ya wagonjwa ikiwemo ununuzi wa dawa.

“MNH ndio hospitali kubwa Tanzania ambapo wataalamu bingwa wa kada nyingi wanapatikana hapa ambapo kwa siku tunaona wagonjwa wa nje kati ya 1,500 hadi 2,000 na waliolazwa takribani 1,300. Asilimia 36 ya wagonjwa hawa ni wa msamaha, kwa hivyo msaada utasaidia hospitali kuelekeza pesa ambazo zingetumika kwenye manunuzi ya luninga kwenda kwenye mahitaji ya wagonjwa,” amesema Prof. Janabi.

Amebainisha kuwa uwepo na luninga katika mazingira ya Hospitali unasaidia kuhabarisha ndugu wanaouguza wagonjwa lakini pia ni sehemu ya tiba kwa baadhi ya wagonjwa.

Kwa upande wake Afisa Mtendaji Mkuu wa Kampuni ya Assemble, Bi. Tabia Massoud amesema kuwa kampuni yake inavutiwa kwa namna MHN inavyopiga hatua kwa kuboresha huduma.

“Muhimbili ni mshirika wetu mkubwa kwa kuwa wateja wetu wengi wanahudumiwa hapa, msaada huu utawanufaisha pia na wateja wetu ambao wananufaika na huduma za matibabu hapa,” amesema Bi. Massoud.

By Jamhuri