Na Mwandishi Wetu, JamhuriMedia, Geita

MAMLAKA ya Mapato Tanzania (TRA) mkoani Geita imewatahadharisha wafanyabiashara wanapotoa risiti za Mashine za Kielektoniki (EFD) kuhakikisha zinakuwa na taarifa kamili na si vinginevyo.

Aidha TRA imewataka wateja wanaponunua bidhaa na kupatiwa risiti ya EFD wahakiki taarifa za risiti hizo ili kuepusha udanganyifu na kuwezesha wafanyabiashara walipe kodi sahihi.

Meneja wa TRA Mkoa wa Geita, Maimuna Khatib ametoa angalizo hilo mjini Geita wakati akizungumuza katika hafla ya uzinduzi wa kampeni ya Tuwajibike inayohamasisha utoaji na uombaji wa risiti.

“Risiti halali za EFD zinatakiwa ziwe na TIN namba, anuani na jina la muuzaj, jina la mnunuzi na ikiwezekana hata TIN namba ya mnunuzi na ionyenshe thamani halisi ya bidhaa.

“Pia ionyeshe muda wa ile risiti ilivyotolewa na kwa sasa tunakumbusha wauzaji na wanunuzi kutimiza wajibu wao kwa kufuata sheria kwa kutoa na kudai risiti.” Amesema Maimuna na kuongeza;

“Madhara ya kutozingatia sheria ni kupata adhabu pamoja na kupata usumbufu usio wa lazima, kutokudai risiti na kutotoa risiti ni kosa kisheria.”

Amesisitiza mfanyabiashara mwenye vigezo vya kutumia mashine ya EFD atakayebainika kutotoa risiti kwa makusudi au kwa kufanya udanganyifu wowote wakati anauza bidhaa atatozwa faini ya Sh milioni 1.5.

Mkuu wa mkoa wa Geita, Martin Shigela amewaagiza viongozi wote wa serikali kuanzia ngazi ya mtaa, kata mpaka halmashauri kusimamia kwa ufanisi kampen ya tuwajibike ili kuongeza mwitikio.

By Jamhuri