Na Andrew Chale, JamhuriMedia, Dodoma

BANDA la Shirika la Farm Africa linalojishughulisha na masuala ya kilimo nchini lilipo ndani Maonesho ya Kanda ya Kati ya Wakulima ‘Nane Nane’ yanayoendelea katika viwanja vya Nzuguni Jijini Dodoma yenye kauli mbiu Kitaifa “Vijana na Wanawake ni Msingi Imara Mifumo Endelevu ya Chakula ” ambapo limekuwa gumzo kufuatia bidhaa mbalimbali na elimu wanayotoa katika banda hilo.

Mapema Jumapili banda hilo pia lilitembelewa na mgeni rasmi Donald Mejitii Mwekiti wa Halmashauri ya Bahi ambapo alipongeza shughuli zinazofanywa na Shirika hilo ikiwemo kuwainua Vijana na Wanawake katika fursa za ajira na kilimo.

“Niwapongeze kwa juhudi zenu kama Farm Africa kwa kushiriki na kuandaa vema maonyesho ya kilimo.
Pia watu watajifunza mengi shughuli zenu mnazozifanya katika kuinua kilimo hapa nchini” amesema Donald Mejitii.

Ambapo pia ameweza kushuhudia bidhaa zitokanazo na zao la Alizeti na Mtama huku pia akivutiwa zaidi na jinsi ya kutengeneza mkaa unaotokana na mashudu ya alizeti. Mkaa huo rafiki wa mazingira na unauzwa kwa bei nafuu.

Mbali na mkaa huo, pia ameifurahia teknolojia ya kupanda mbegu ya mazao kama Alizeti na Mtama kwa kutumia mashine (planter) na pia uzalishaji wa mbegu za QDS (UMBEGU) unaofanywa na wakulima wenyewe kwa kuongeza tija kwenye kilimo cha Alizeti na Mtama kwa Kanda ya Kati.

Kwa upande wake Afisa kutoka Farm Africa, Meshack Panga ameeleza kuwa, wanafanya shughuli mbalimbali ikiwemo kuinua vijana na Wanawake katika miradi tofauti katika Kilimo.

“Shirika limefanikiwa na miradi mbalimbali ikiwemo mradi wa Vijana Kilimo Biashara unaofadhiliwa na Shirika la Mpangowa wa Chakula WFP.

Lakini pia mradi wa Kilimo Himilivu cha zao la Mtama unaofadhiliwa na Serikali ya Ireland kupitia Ubalozi wake hapa Tanzania.” amesema Meshack.

By Jamhuri