Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Mheshimiwa Innocent Lugha Bashungwa (Mb) amewakabidhi Magari Mapya, Jenerali George Marwa Waitara (Mstaafu) pamoja na Jenerali Robert Philemon Mboma (Mstaafu) tukio lililofanyika Ofisi za Wizara, Mtumba Jijini Dodoma.

Akikabidhi Magari hayo, Mheshimiwa Waziri Bashungwa amesema, kuwapatia Majenerali Wastaafu Magari ni sehemu ya maelekezo ya Mheshimiwa Rais na Amiri Jeshi Mkuu, kwamba tuwapatie Magari mapya ambayo yanatengenezeka na spea zake zinapatikana kwa urahisi.

Aidha Waziri wa Ulinzi na JKT amewahakikishia Majenerali kwamba, yeye na watendaji wa Wizara anayoiongoza wataendelea kuwajali na kuwapa stahili, kwani Taifa bado linawahitaji na ni hazina kwa Nchi yetu.

Naye, Katibu Mkuu wa Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Dkt. Faraji Kasidi Mnyepe, amewahakikishia Majenerali hao kuhusu huduma stahiki ya Magari hayo ikiwemo service yake, kwamba huduma hizo zipo kwa mujibu wa sheria, hivyo zitaendelea kugharimiwa na Serikali na mara wapatapo hitilafu wasisite kutoa taarifa.

Akitoa shukrani, Jenerali George Marwa Waitara (Mstaafu) amemshukuru Mheshimiwa Rais na Amiri Jeshi Mkuu “Naomba ufikishe shukrani hizi kwa Mhe. Rais, mwambea tumefurahi na tumeona jinsi gani anavyotujali wastaafu” alimweleza Mheshimiwa Waziri.

Naye Jenerali Robert Mboma (Mstaafu), pamoja na shukrani, amempongeza Mheshimiwa Rais, Dkt Samia Suluhu Hassan kwa uongozi wake mzuri wa Serikali ya Awamu ya Sita na kumtakia kila la heri na mafanikio katika kuliongoza Taifa letu.

By Jamhuri