Na Mwandishi Wetu, JamhuriMedia, Manyara

Chama Cha Mapinduzi (CCM), kupitia kwa Naibu Katibu Mkuu wa CCM, Bara, Anamringi Macha, kimekabidhi msaada wa vitu vyenye thamani ya Tsh. 10 milioni, ‘kuwashika mkono’ waathirika wa maafa yaliyosababishwa na mafuriko ya maji na matope, huko wilayani Hanang. 

Akikabidhi msaada huo kwa waathirika hao mbele ya Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Kassim Majaliwa Majaliwa, mjini Katesh, Macha amesema kuwa Chama Cha Mapinduzi kiko pamoja na wananchi wote walioathiriwa katika kipindi hiki kigumu, huku akiishukuru Serikali kwa namna ambavyo imejitahidi kushughulikia athari za maafa hayo, tangu baada ya taarifa kutoka. 

“Mheshimiwa Waziri Mkuu…Watanzania tumepokea kwa masikitiko makubwa sana kuhusiana na maafa haya. Nawapeni pole sana. Na kipekee nichukue nafasi hii kuishukuru Serikali yetu kwa jinsi ambavyo tangu taarifa hizi zitokee mmekuwa mkijitahidi. 

“Tunamshukuru sana Rais wetu Mheshimiwa dokta Samia Suluhu Hassan ambaye pamoja na kwamba yuko mbali, ameshirikiana nasi hapa katika kutoa maelekezo ambayo wewe Waziri Mkuu na wasaidizi wako mmeyapokea na kuyatekeleza. Tuendelee kuwaomba wananchi tuendelee kushirikiana. Na kuziomba taasisi zote za Serikali na taasisi binafsi tuendelee kushirikiana katika wakati huu wa maafa.”

“Maafa ni yetu wote. Hayana dini, hayana kabila, hayana Chama, tushikamane katika kuwasaidia wenzetu kila mmoja kwa kadri anavyoweza au kwa jinsi Mwenyezi Mungu alivyomsaidia,” amesema Ndugu Macha, akitoa wito kwa Watanzania kuendelea kumuomba na kumtegemea Mungu katika wakati huu mgumu. 

Msaada ambao Naibu Katibu Mkuu wa CCM Bara, Ndugu Macha amekabidhi kwa waathirika, kwa ajili ya kushikamana nao, ni pamoja na mchele, maharage, maji ya kunywa, unga na sabuni.