Na Dotto Kwilasa, JamhuriMedia,Dodoma.

Kutokana na kuwepo maneno mengi ya kubeza Mkataba wa uwekezaji wa Bandari,hatimaye Askofu Wilbard Ringia wa Kanisa la Mizaituni miwili,Pentecoste Assemblies (MMPA) amejitokeza na kuwataka Watanzania kuwa watulivu na wenye kuheshimu mamlaka ili mambo mengine yaendelee.

Askofu Ringia ameyasema hayo leo Julai 16,2023 Jijini hapa wakati akizungumza na waandishi wa Habari kuhusiana na uwekezaji huo ambapo amesema maneno mengi yanayobeza hayautukuzi utukufu wa Mungu.

Amesema Mamlaka zote ulimwenguni huwekwa na Mungu hivyo Watanzania hawapaswi kuwa na hofu na Serikali iliyopo madarakani kwani kila jambo linalotokea limepangwa na Mungu.

“Kila mwanadamu ameumbwa na mungu,hata kuwepo madarakani kwa Rais wetu Samia Suluhu Hassan pia ni mipango ya Mungu hivyo hatuna sababu ya kumlalamikia kwani yote anayoyafanya yanatokana na Mwenyezi Mungu kwa kuwa tunaamini Mungu humtengeneza mtu kuwa Kiongozi tangu anapokuwa tumboni mwa mamaye,”amesisitiza

Pamoja na hayo amesisitiza kuwa mamlaka ya Mungu huanzia duniani kupitia viongozi wakuu wananchi hivyo Watanzania hawana haja ya kuwa na shaka na maamuzi yoyote yanayotolewa na viongozi hao.

“Tuiachie Serikali ifanye maamuzi na hatma ya maendeleo yetu kwa sababu inao wataalamu wengi ,nataka niwaambie watanzania kuwa Serikali huwa haikurupuki badi huanza kufanya upembuzi wa mambo kupitia wataalamu wake kabla ya kutoa suluhu,msiwe na wasiwasi,”amesema na kuongeza;

Haisaidii kuleta maneno maneno uwekezaji ni jambo muhimu mno kila mtu anajua, ningeshauri tuheshimu mamlaka ya nchi na kufuata maelekezo ya viongozi wa dini ili kuwa na maarifa zaidi,najua yote haya yanatokea kwa kuwa watu wengi hawana maarifa , watu wanapotea kwa sababu hawajui maandiko,hebu kila mmoja asimame kwenye nafasi yake ili tuungane kuijenga nchi yetu,”amesema.

Askofu huyo pia ametumia nafasi hiyo kuwa sasa Watanzania kukataa kuishi kwa kusikiliza hadidhi za uongo zinazokwamisha maendeleo na badala yake wafuate muongozo wa Serikali inavyotaka.

“Si adabu wala heshima kumdharau Rais tumpe nafasi ashughulikie uchumi wetu Mungu hataki fujo wala kudharauli,”amesisitiza

By Jamhuri