Bendi ya muziki wa dansi ya Extra Bongo ya jijini Dar es Salaam, imesema kuwa inajivunia mafanikio ambayo imekuwa ikiyapata tangu kuanzishwa kwake.

Akizungumza na JAMHURI Dar es Salaam hivi karibuni, kiongozi wa bendi hiyo, Ally Choki, alieleza anafurahishwa kwake na jinsi bendi yake inavyofanya vizuri katika tasnia hiyo. Hatua hiyo imesababisha bendi hiyo kuongeza idadi ya mashabiki wa muziki wa dansi nchini.

 

“Ni muda mrefu sasa bendi yangu imeingia sokoni na imekuwa ikijiongezea idadi ya mashabiki, hali hii inanipa matumaini ya kuendelea kuwapo katika fani hii,” alisema Choki.

 

Alisema kuongezeka kwa idada ya mashabiki kunatokana na kujitokeza kwa wingi kwa wapenzi wa bendi hiyo wakati wa maonesho mbalimbali yanayofanywa na bendi hiyo ndani na nje ya Dar es Salaam.

 

Hivi karibuni, bendi hiyo ilimtangaza Richard Maarifa kuwa amerejea katika bendi hiyo. Maarifa ni kati ya wanamuziki walioanzisha bendi hiyo kabla haijavunjika na kuundwa tena.

Kuja kwa Maarifa kumetafsiriwa kama hali ya kuziba pengo la mwanamuziki Rogatti Hegga, ambaye kwa sasa ameachana na bendi hiyo na kuungana na Hamis Kiyumbi ‘Amigolas’ Baba Diana aliyeachana na Twanga Pepeta.

 

Wasanii hawa tayari wametangaza kuanzisha bendi yao ambayo pia itamshirikisha mwanamuziki machachari Msafiri Diouf aliyekuwa Twanga Pepeta. Wasanii hao katika nyakati tofauti wamenukuliwa na vyombo vya habari wakijinadi kuwa wanataka kuingia sokoni kwa staili ya pekee ambayo itawapatia mashabiki.

 

Wachambuzi wa muziki kwa nyakati tofauti wamesema ujio wa wanamuziki hao kutika tasnia ya muziki wa dansi itaongeza ushindani.

 

Hatua hiyo itasababisha bendi kongwe na maarufu za muziki wa dansi nchini kujizatiti upya ili kukabiliana na ushindani huo, ambao utawapa nafasi zaidi wapenzi wa muziki wa dansi kuamua kufanya uchaguzi katika bendi itakayofanya muziki bora na si bora muziki.

 

0783 106 700

By Jamhuri