Na Mwandishi Wetu, JamhuriMedia

Hospitali ya Rufaaa ya Mkoa wa Simiyu imeanza kupokea vifaa tiba mbalimbali kutoka Bohari ya Dawa (MSD) Kanda ya ziwa, kwaajili ya kuanza kutoa huduma za kibingwa kwa akina Mama wajawazito na watoto.

Hatua hiyo inatajwa kuwa itaondoa kabisa adha iliyokuwepo katika mkoa huo, ambapo akina mama wajawazito na watoto waliohitaji huduma hizo walilazimika kupelekwa katika hospitali ya Rufaa ya kanda Bugando, Mkoani Mwanza.

Akipokea vifaa hivyo ambavyo ni vitanda 9 vyenye thamani ya shs. mil.23, kwa ajili ya huduma za kibingwa kwa akina mama wajawazito, Mganga Mfawidhi wa Hospitali hiyo Dkt. Athanas Ngambakubi, ameishukuru serikali kupitia MSD kwa kurahisisha na kuwahisha upatikanaji wa vifaa hivyo.

Dkt. Ngambakumbi amesema kuwa malengo ya Rais Samia Suluhu Hassan ya kuhakikisha wananchi wanapata huduma za Afya kwenye maeneo yao, yanakwenda kukamilika katika Mkoa wa Simiyu.

“Awali mama mjamzito akihitaji huduma za kibingwa ililazimika kukimbizwa Bugando, Kilometa zaidi ya 150, lakini kwa sasa MSD wameleta hivi vifaa na vingine tayari wameishaleta, ndoto ya Rais Samia sasa inakwenda kukamilika,” Alisema Dkt. Ngambakubi.

“ MSD wameleta vifaa hivi na vimekuja kwa wakati, jengo la akina mama na wajawazito nalo lipo katika hatua ya mwisho kukamilika, hivyo ndani ya mwezi mmoja huduma hii itapatikana hapa Simiyu,” alisisitiza Dkt. Ngambakubi.

Dkt. Ngambakubi pia ameipongeza MSD kwa huduma ambayo wamekuwa wakitoa katika hospitali hiyo, ambapo ameeleza mbali na vifaa hivyo wamekuwa wakipokea dawa pamoja na mahitaji mengine kwa wakati.

Kwa upande wake Mratibu wa Huduma za Tiba katika Hospitali hiyo Dkt. Seleman Athumani, amesema kuwa MSD kuleta vifaa hivyo, huduma za Mama na mtoto zikiwemo za kibingwa zinakwenda kuimarika katika hospitali hiyo.

Ameongeza kuwa ujenzi wa jengo la Mama na Mtoto ujenzi wake umefikia asilimia 95, ambapo mafundi wanaendelea na ukamilishaji wa baadhi ya maeneo huku akibainisha kuwa ndani ya mwezi mmoja jengo litaanza kufanya kazi.

“ Tunashukuru MSD kwa vifaa hivi ambavyo wameleta kwani vitaongeza chachu katika utoaji wa huduma, kwakuwa huduma hii, imekua tamanio letu la muda mrefu, kilichobaki ni vifaa vyenyewe kufungwa, na ujenzi wa jengo upo katika hatua ya mwisho, tunategemea ndani ya mwezi mmoja tutaanza kutoa huduma katika jengo hili,” amesema Dkt. Athumani

By Jamhuri