Na A/INSP Frank Lukwaro

Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini IGP Camillus Wambura amewataka Watendaji wa Dawati la Jinsia na Watoto kutoa huduma bora kwa wahanga wa vitendo vya ukatili wanaoripoti matukio ya ukatili katika vituo vya Polisi ili kujenga taswira chanya ya Jeshi la Polisi kwa jamii jambo ambalo litasaidia kutoa haki kwa wahanga wote wa matukio hayo.

Mkuu wa Jeshi la Polisi Nchini IGP Camillius Wambura akiingia katika ukumbi wakati wa ufungaji wa kikao cha mwaka cha Watendaji wa Dawati la Jinsia na Watoto kilichokuwa kikifanyika Jijini Tanga kwa lengo la kufanya tathmini kwa mwaka 2022 na kuweka mikakati kwa mwaka 2023. Kulia ni Kamishna wa Polisi Jamii Faustine Shilogile (Picha zote na Jeshi la Polisi)

IGP Wambura ameyasema hayo Jijini Tanga wakati akifunga kikao cha Watendaji wa Dawati la Jinsia na Watoto kutoka mikoa ya Tanzania Bara na Zanzibar kilichokuwa kikifanyika jijini humo kwa siku tatu kwa lengo la kufanya tathmini kwa mwaka 2022 na kuweka mikakati kwa mwaka 2023.

Aliwataka watendaji hao kuhakikisha kuwa kunaendelea kuwepo na usiri katika kushughulikia wahanga wa vitendo vya ukatili nchini na kwa wanaofanya vitendo hivyo waweze kufichuliwa ili lengo la kukomesha vitendo hivyo liweze kutimia.

“Kwa takwimu zilizopo bado watendaji mna kazi kubwa ya kufanya huko mikoani kwa kuendelea kutoa elimu na kutowaonea huruma na muhali wahalifu wote wa vitendo vya ukatili wa kijinsia” amesema IGP Wambura.

Kwa upande wake Kamishna wa Polisi Jamii Faustine Shilogile amesema kikao hicho hufanyika kila mwaka kwa lengo la kufanya tathmini na kubaini mafanikio na changamoto ambazo huwekewa mikakati ili kuendelea kukomesha vitendo vya ukatili nchini.

Viongozi mbalimbali wakifuatilia ufungaji wa Kikao cha mwaka cha Watendaji wa Dawati la Jinsia na Watoto kilichokuwa kikifanyika Jijini Tanga kwa lengo la kufanya tathmini kwa mwaka 2022 na kuweka mikakati kwa mwaka 2023.

Aidha, amesema Kumekuwepo na changamoto mbalimbali katika utendaji wa madawati nchini ikiwemo ukosefu wa majengo yenye vigezo vya Dawati katika baadhi ya vituo vya Polisi ambapo kwakushirikiana na wadau wataendelea kuboresha katika eneo hilo.

Naye Mwakilishi wa Shirika la LSF Bi. Jane Matinde alisema shirika hilo litaendelea kufadhili mafunzo kwa watendaji hao ili kuwa na watendaji wenye weledi katika dawati ambalo limekuwa mkombozi kwa wanajamii wa Tanzania ambao wamekuwa wakifanyiwa vitendo vya ukatili.

Mkuu wa Jeshi la Polisi Nchini IGP Camillius Wambura akizungumza katika  ufungaji wa kikao cha mwaka cha Watendaji wa Dawati la Jinsia na Watoto kilichokuwa kikifanyika Jijini Tanga kwa lengo la kufanya tathmini kwa mwaka 2022 na kuweka mikakati kwa mwaka 2023.

By Jamhuri