Rais Mstaafu Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete akiambatana na mke wake Mama Salma Kikwete wamezuru jamii ya Wahadzabe wanaoishi katika Kijiji cha Endamagha kilichopo Kata Tarafa ya Eyasi, Wilaya ya Karatu.

Katika ziara yao hiyo Dkt. Kikwete na mkewe wamepata fursa ya kujifunza mambo mbalimbali ya mila na desturi za jamii hiyo ya Wahadzabe hususan njia zao za asili za kutafuta na kuhifadhi vyakula, malezi ya watoto, makazi yao, nk.

Pamoja na mambo mengine waliweza pia kuongea kwa kina na wanajamii hao kuhusu changamoto zinazowakabili kama vile changamoto ya upatikanaji wa elimu kutokana na mfumo wao wa maisha wa kuhamahama, uvamizi wa makabila mengine katila maeneo yao ya asili hali inayotishia mtindo wao wa maisha pamoja na upatikanaji wa huduma nyingine muhimu za kijamii.

Dkt. Kikwete alitumia fursa hiyo kuwapongeza wenyeji wake kwa kuendelea kudumisha mila na desturi zao huku wakitambua na kuzingatia umuhimu wa kuwapeleka watoto wao shule ili kupata elimu itakayokuja kuwasaidia katika maisha yao ya baadaye.

Aidha, aliwataka viongozi wa Serikali walioambatana naye kuzidisja ukaribu na jamii hiyo ili kusikiliza, kuzielewa na kuzitafutia ufumbuzi changamoto za kipekee zinazoikabili jamii hiyo.

By Jamhuri