Shirika la habari la serikali nchini Korea Kaskazini limesema kuwa kiongozi wa taifa hilo Kim Jong Un amekubali mwaliko wa Rais wa Marekani Donald Trump wa kufika Washington.

Kiongozi huyo alipewa mwaliko wakati wa mkutano wa historia baina ya wawili hao nchini Singapore Jumanne.

Kim pia alimwalika pia Trump kutembelea Pyongyang.

“Viongozi ao wawili wakuu walikubali mwaliko wa kila mmoja,” shirika la KCNA limeripoti.

Kenye tamko lake la kwanza kabisa tangu kutokea kwa mkutano huo, Bw Kim amenukuliwa akisema kwamba kuna haja ya “dharura” ya kusitisha “hatua za kijeshi za uchokozi zinazokera kati ya mataifa” hayo mawili.

Alisema nchi zote mbili zinafaa “kujitolea kujizuia kufanya uchokozi” na “kuchukua hatua za kisheria na kitaasisi kuhakikisha hilo linafanyika”, KCNA wameripoti.

Wachanganuzi wanasema kuwa ni nafasi nzuri ya kuendeleza uhusiano baina ya nchi mbili, lakini wakosoaji wanasema kuwa hii huenda ikasababisha majaribio ya mapinduzi ya serikali Korea kaskazini.

Hakuna tarehe iliyotolewa kwa ziara hiyo lakini katika mahojiano na shirika la habari la Fox News, Trump alikuwa amesema baadaye kwamba Kim anakaribishwa kuzuru White House wakati wowote ule utakaofaa.

Hayo yakijiri, Marekani imewahakikishia washirika wake katika eneo la Asia Mashariki kwamba itatekeleza majukumu yake ya kuwalinda.

Hii ni baada ya Rais Trump kukubali kufutilia mbali mazoezi ya pamoja ya kijeshi kati ya Marekani na Korea Kusini baada ya kukutana na Bw Kim.

Korea Kaskazini imekuwa ikiitaka Marekani kusitisha mazoezi hayo yanayofanyika kila mwaka kwa muda mrefu.

Uhasama kati ya Marekani na Korea Kaskazini ulikuwa ukizidi kila mazoezi hayo yanapoanza.

Hatua ya Trump kukubali kusitisha mazoezi hayo ilionekana kama ‘kubadilisha msimamo pakubwa’ kwa Marekani na iliwashangaza washirika wa Marekani katika kanda hiyo.

Mazoezi hayo ambayo pia huitwa “michezo ya kivita” hufanyika nchini Korea Kusini na kuwashirikisha wanajeshi wa Korea Kusini na wanajeshi wa Marekani walio nchini humo.

Rais wa Korea Kusini Moon Jae-in alizungmza na Rais Trump kwa njia ya simu baadaye Jumanne, lakini taarifa rasmi iliyotolewa baada ya mazungumzo hayo haikugusia mazoezi hayo ya pamoja ya kijeshi, Reuters wamesema.

Siku iliyotangulia mkutano wa Jumanne, Waziri wa Ulinzi wa Marekani Jim Mattis alikuwa amewaambia wanahabari kwamba hakuwa anaamini kiwango cha wanajeshi wa Marekani rasi ya Korea kingezungumziwa.

Alipouliwa iwapo angejua kama mazungumzo kama hayo yalikuwa yameandaliwa, alisema, “Ndio, bila shaka ningejulishwa.”

By Jamhuri