Mkutano wa kihistoria kati ya Rais wa Marekani Donald Trump na Kiongozi wa Korea kaskazini Kim Jong Un umefanyika nchini Singapore.

Wawili hao walikutana kwanza kwa dakika 38 kwa mujibu wa ikulu ya White House, na walikuwa ni wawili hao pekee na wakalimani wao.

Mkutano huo ulianza kwa viongozi wawili kusalimiana kwa tabasamu na kisha kuelekea ukumbi wa maktaba ya Cappela Hotel kwa ajili ya sehemu ya kwanza ya mkutano wa ana kwa ana baina yao.

Bw Trump amesema wawili hao walipiga hatua kubwa na kwamba karibuni kutakuwa na sherehe ya kutia saini nyaraka ya makubaliano.

Wamekuwa wakijadiliana kuhusu njia za kupunguza uhasama rasi ya Korea na kati ya Korea Kaskazini na Marekani na pia jinsi ya kupunguza silaha za nyuklia.

Hata hivyo, haijabainika ni nini kitakuwepo kwenye waraka ambao watautia saini.

Trump alisikika akisema kuwa anatarijia makubaliano mazuri katika mkutano huku Kim akisema kuwa haikuwa rahisi kufika hapo.

Mkutano uliokua ukisubiriwa kwa hamu na ghamu ulifanyika katika Hotel ya Capella katika kisiwa cha utalii cha Sentosa.

Viongozi hawa wakiingia katika mkutano walionekana wenye tabasabu, na kusalimiana kwa kushikana mikono, na baadae Kim Jong Un alimshika bega Trumpa kisha wakaanza kuzungumza kwa msaada wa wakalimani wao.

Baadaye washauri na maafisa mbalimbali walitarajiwa kuingia kuendelea na mkutano huku suala la nyuklia likitarijiwa kujadiliwa kwa kina na haijajulikana bado makubaliano yatakua yapi.

Akizungumza kabla ta mkutano , katibu mkuu wa umoja wa mataifa, Antonio Guterres amesema kuwa umoja wa mataifa utatoa msaada wowote wa kuhamasisha makubaliono katika mkutano huo.

”Viongozi wawili, wanajaribu kujadiliana jinsi ya kufikia makubaliano ambayo yalileta sana utata mwaka jana, amani na suala la kusitisha nyuklia ndio vinabaki kuwa lengo kuu, kama nilivyowaandikia mwezi uliopita kutahitajika ushirikiano wa hali ya juu na kutakua na changamoto za hapa na pale katika makubaliano, Marekani wanatakiwa kusimamia kwa vyovyote,” alisema Guterres.

Mcheza kikapu wa zamani wa NBA, Dennis Rodman amefika Singapore asubuhi ya leo kwa ajili mkutano huo, Rodman ambaye ni rafiki wa kiongozi wa Korea Kaskazini amesema kuwa anafurahia kufika na kushuhudia mkutano huo wa kihistoria.

Uhusiano wa viongozi hawa wawili umepitia kwenye milima na mbonde kwa kipindi cha miezi 18 iliyopita, wakirushiana matusi na kutishiana vita kabla ya uhusiano wao kuchukua mkondo mwingine na kuamua wawili hao kukutana.

Mwaka wa kwanza wa Trump katika kiti cha urais ulianza kwa mvutano mkubwa na kurushiana maneno huku Kim naye akiendeleza majaribio ya silaha za nuklia na kukiuka ilani ya kimataifa.

Rais wa Marekani aliapa kupambana ikiwa Pyongyang itaendelea kuitishia Marekani, wote wakipeana majina ya kukebehi.

Korea Kaskazini iliendelea kukaidi na kufanya jaribio la nuklia la sita mwezi Septemba mwaka 2017.

Baadae Kim alitangaza kuwa nchi yake imefanikiwa mpango wake wa kua taifa la nuklia, likiwa na silaha zinazoweza kuifikia Marekani.

Lakini mwanzoni mwa mwaka 2018, Korea Kaskazini ilianza kuboresha mahusiano na Korea Kusini kwa kupeleka timu na ujumbe kwenye michuano ya Olimpiki mjini Pyeongchang.

Mwezi Machi, Donald Trump aliushangaza ulimwengu kwa kukubali mwaliko kutoka kwa Kim wa kukutana ana kwa ana.

Tangu wakati huo, njia ya kuelekea mkutano huu ikawa yenye changamoto, Trump akiahirisha kabisa.Lakini sasa viongozi hao watakaa pamoja.

Singapore ni nchi ya tatu ambayo Kim Jong-un ameitembelea tangu alipokuwa Kiongozi mwaka 2011.

safari yake ya kwanza ilikuwa nchini China mwezi Machi na mwezi Aprili akawa kiongozi wa kwanza wa Korea Kaskazini kutembelea Korea Kusini ambapo alikutana na Moon Jae-in.

By Jamhuri