Makamu Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Abdulrahaman Kinanaa amewashauri na kuwakumbusha wanaiasa wa upinzani kuheshimu fursa ya maridhiano ya kisiasa iliyotolewa na Rais Dk. Samia Suluhu Hassan.

Amesema lugha za matusi, kejeli na dharau dhidi kiongozi wa nchi zinapaswa kuepukwa ili kutoa fursa ya kuendeleza maridhiano na kuijenga Tanzania kwa pamoja.

Kinana ameyasema hayo jana mjini Tabora wakati akizungumza na wananchi katika mkutano wa hadhara alipokuwa akihitimisha ziara yake ya kikazi katika mikoa ya Dodoma, Manyara, Mara, Simiyu na Tabora kukagua utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya 2020-2025 na uhai wa Chama.

“Niwasihi ndugu hatukatai mtoe hoja, hatukatai mseme yale mnayotaka kusema lakini semeni kwa uungwana, zungumzeni kwa busara, jengeni hoja.

“Kusema Rais ana akili za matope au kusema Rais ameuza bandari, wewe sema mkataba huu haujakaa vizuri, utaeleweka, toa hoja kwa nini hauajakaa vizuri, upande wa pili watasema umekaa vizuri, lakini ukisema mkataba huu hata kichaa hawezi kuubali, maana nyingine unatuambia sisi sote ni vichaaa” amesema.

Kinana alitumia fursa hiyo kuelezea mchakato wa kupata maridhiano ambayo yametoa fursa ya wananchi wakiwamo wanasiasa kuwa na uhuru wa kutoa maoni.

“Kabla ya hapo mtakumbuka Mwenyekiti wa Chadema Freeman Mbowe alikuwa jela, Rais (Dk . Samia) kabla ya kesi haijamalizika akaamua kumwalika Ikulu…wakazungumza, wakakubaliana kwamba tujenge amani na umoja, hatimaye mazungumzo ya Chamwino yakazaliwa. Rais akaunda timu ya watu 10, watano CCM na watano Chadema.

“Leo nayasema haya kwa sababu mimi ni Mwenyekiti kwa upande wa CCM katika mazungumzo hayo ya maridhiano. Mwenyekiti mwenzangu Freeman Mbowe yeye aliongoza upande wa pili na walikuja na hoja 15,” amesema.

By Jamhuri