Tayari mataifa yatakayoshiriki fainali za Kombe la Dunia huko Qatar baadaye mwaka huu yamekwisha kufahamika, huku nafasi chache zilizosalia zikitarajiwa kujazwa Juni 13 na 14 mwaka huu katika hatua ya mchujo (inter-confederation play-offs); pamoja na mechi kati ya Ukraine na Scotland nayo ikisogezwa hadi Juni. 

Hata hivyo, tayari makundi yamekwisha kupangwa kwa mechi za awali za fainali hizo. Mataifa shiriki ni haya hapa: 

Taifa Mwenyeji

Tayari Qatar wamekwisha kuthibitishwa kushirikikwa sababu za wazi kabisa. Lakini huenda hii ikawa mara ya mwisho kwa miaka kadhaa ijayo kushuhudia taifa moja likipita moja kwa moja, kwa kuwa wenyeji wa fainali za mwaka 2026 ni mataifa matatu; Marekani, Canada na Mexico huku kukiwa na maombi mengi kutoka kwa mataifa kadhaa yakitaka kuandaa kwa pamoja fainali za mwaka 2030. 

Ulaya 

Mataifa ya mwisho ya Ulaya kuchukua nafasi Kombe la Dunia 2022 wiki iliyopita ni Poland na Ureno. Kwa hiyo kutoka Ulaya kutakuwa na mataifa 13 yafuatayo: 

  • Ujerumani
  • Denmark
  • Ufaransa
  • Ubelgiji
  • Croatia
  • Hispania
  • Serbia
  • England
  • Uswisi
  • Uholanzi
  • Poland
  • Ureno na ama
  • Scotland au Ukraine au Wales

Amerika Kusini

Bara hili linawakilishwa na mataifa matano; moja miongoni mwa hayo likilazimika kucheza mchujo.  Mataifa hayo ni: 

  • Brazil
  • Argentina
  • Ecuador na
  • Uruguay huku
  • Peru ikipitia kwenye mchujo

Afrika

Bra la Afrika linawakilishwa na mataifa matano yaliyopenya kwenye chekeche la nguvu. Mataifa hayo ni: 

  • Senegal
  • Cameroon
  • Ghana
  • Morocco na
  • Tunisia

Amerika Kaskazini

Zimechezwa raundi tatu huku mataifa manane yakigombea nafasi tatu za moja kwa moja na nafasi moja inayopatikana kwa njia ya mchujo. Wawakilishi wa bara hili ni: 

  • Canada
  • Mexico
  • Marekani wakati 
  • Costa Rica italazimika kwanza kupambana na New Zealand katika mechi za mchujo

Asia

Mataifa manne yamepita moja kwa moja huku taifa moja likilazimika kucheza mechi ya mchujo kupata nafasi ya kushiriki fainali za Kombe la Dunia. Mataifa yaliyopita ni haya hapa:

  • Korea Kusini
  • Iran
  • Japan
  • Saudi Arabia
  • Australia/United Arab Emirates zitapitia mechi za mchujo kupata nafasi moja iliyosalia

By Jamhuri