KOCHA wa timu ya Tanzania, Taifa Stars, M-Cameroon, Emmanuel Amunike, amekutana na wachezaji Simba aliowaondoa kwenye kikosi chake baada ya kuchelewa kuripoti kambini.

Baada ya kukutana nao, Ofisa Habari wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Clifford Ndimbo ametoa taarifa kuwa suala hilo limekwisha na kwamba hakuna kitakachozuia nyota hao kuitwa tena Stars kama tu wataonyesha kiwango kizuri kwenye klabu yao.

Ndimbo ameeleza kuwa Amunike ameshamalizana na wachezaji wa Simba na atawaita tena endapo wataonesha kiwango kizuri ambacho kitamshawishi wakiwa kwenye klabu yao.

Licha ya kusamehewa, wachezaji hao wataukosa mchezo wa kuelekea kufuzu AFCON dhidi ya Uganda, Septemba 8 2018 huko Kampala.

Nyota hao sita watakosekana kutokana na nafasi zao kujazwa na wachezaji wengine ambao tayari wameshaanza mazoezi jana kwenye Uwanja wa Boko Veterani uliopo pembezoni kidogo mwa jiji la Dar es Salaam.

By Jamhuri