Na Mwandishi Maalum, JamhuriMedia, Mwanza

Madaktari wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Mwanza Sekoutoure wamefanikiwa kufanya upasuaji na kuondoa Jiwe ndani ya kibofu cha mkojo kwa mwanamke mwenye umri wa miaka 48.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa hospitalini hapo jiwe hilo lenye uzito wa gramu 800 lililomsumbua mhusuka kwa zaidi ya miaka mitatu.

Akizungumza leo Aprili 18, 2024 na Daktari Bingwa wa Upasuaji katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Mwanza Sekoutoure Dkt. Jackson Chiwaligo amesema hiyo ni mara ya kwanza kufanya upasuaji kama huo.

Dkt. Chiwaligo ameeleza kuwa mgonjwa huyo alifika Hospitali ya Sekoutoure akiwa na changamoto ya kupata maumivu makali sehemu ya chini ya tumbo kwa zaidi ya miaka mitatu.

“Baada ya vipimo aligundulika kuwa na uvimbe mkubwa sehemu ya kibofu cha mkojo ulisababisha kufanyiwa upasuaji na kuondoa lenye uzito wa Gramu 800”, amebainisha Dkt. Chiwaligo.

Dkt. Chiwaligo ambaye aliwaongza madakatafi wenzake amesema uwepo wa jiwe kwenye kibofu ni mkusanyiko wa madini ya chumvi ambayo hukauka na kusababisha uvimbe kutokea katika kibofu cha mkojo.

Kuhusu dalili za awali za tatizo hilo Dkt. Chiwaligo amesema dalili mbalimbali zinazosababisha ugonjwa huo kuwa ni pamoja na kukojoa mkojo uliochanganyikana na damu, maumivu makali chini ya tumbo na kushindwa kuzuia mkojo.

“Namna ya kujikinga na ugonjwa huu ni kwenda haja ndogo kwa wakati pale unapoipata na kunywa maji ya kutosha kwa wakati ” , ameeleza Dkt. Chiwaligo

Dkt. Chiwaligo ametoa wito kwa jamii kuwa na utaratibu wa kufika hospitalini kupata huduma za vipimo na kuwa na mtindo bora wa maisha ili kuepuka changamoto ya magonjwa kama hayo.  

By Jamhuri