MBUNGE wa Jimbo la Singida Kaskazini, Ramadhan Ighondo, amesema baadhi ya wataalamu wa ardhi mkoani Dodoma, wamejigeuza madalali na wanashiriki kunyang’anya wananchi wanyonge ardhi.

Akichangia bungeni hotuba ya makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi mwaka 2023/24, leo bungeni mjini Dodoma, amesema baadhi ya maofisa ardhi mkoani Dodoma wamejigeuza madalali wa ardhi.

Amesema maofisa hao wamekuwa wakiwapiga danadana wananchi na wanawanyima haki wanayostahili na kwamba hali ya watendaji wao inamchafua Waziri Silaa, ambaye amekuwa akifanya kazi kubwa tangu alipoteuliwa kuongoza wizara hiyo.

Amesema ingawa baadhi ya watumishi wa Idara ya ardhi waliondolewa mkoani Dodoma, lakini bado vimelea vipo na kwamba ana kesi tatu zinazohusu masuala ya migogoro ya ardhi na atampatia Waziri Silaa azifanyie kazi.