MHASIBU WA SIMBA KIKAANGONI

Shirikisho la soka Tanzania TFF imewapeleka kwenye kamati ya maadili viongozi wanne kwa kughushi na udanganyifu.

Viongozi walioshitakiwa kwenye kamati ya maadili ni msimamizi wa kituo cha Mtwara Dunstun Mkundi, katibu wa chama cha soka mkoa wa Mtwara Kizito mbano, mhasibu msaidizi wa klabu ya Simba Suleiman kahumbu na katibu msaidizi wa klabu ya Ndanda FC ya Mtwara Selemani Kacheche.

TFF inawashitaki viongozi hao kwa makosa ya kughushi pamoja na udanganyifu wa mapato kwenye mchezo namba 94 kati ya Ndanda FC ya Mtwara dhidi ya Simba ya Dare s Salaam iliyochezwa Disemba 30, 2017 kwenye uwanja wa Nangwanda Sijaona, Mtwara.

Kwa tuhuma za hizo viongozi hao watatakiwa kufika mbele ya kamati Januari 18, 2018.

Kamati ya maadili iko chini ya Mwenyekiti Wakili Hamidu Mbwezeleni, makamu Mwenyekiti Wakili Steven Zangira, wajumbe ni Glorious Luoga, Walter Lungu na Amin Bakhresa.