Mahakama Wilayani Lushoto mkoani Tanga mwishoni mwa wiki hii imewatia hatiani watuhumiwa 3 ambao ni Hassan Kashamba, Elihudi Andrew na Godson Kitau kwa makosa mawili ya kukutwa na kijihusisha (Possession and Dealing) na nyara za serikali ambazo ni meno matano ya Tembo kinyume na sheria.

Hakimu Mkazi Mfawidhi Mkuu wa mahakama hiyo Rose Andrew Ngoka amewahukumu kwenda jela miaka 40 kila mmoja kwa makosa yote mawili huku kila kosa likichukua miaka 20.

Watuhumiwa hao licha ya kukutwa na meno matano ya tembo yenye thamani ya zaidi ya shilingi milioni 104, pia walikamatwa na pikipiki 2 aina ya Kinglion zenye usajili namba MC 152 CCQ na MC BWQ zilizokuwa zikitumika katika kutenda uhalifu huo.

Waendesha mashtaka kwa upande wa serikali ambao ni Wakili Mwandamizi Bw. Peter Kusekwa akisaidiana na waendesha Mashtaka wa TANAPA Bw. Samwel Magoko na Flavian Kalinga waliieleza Mahakama hiyo kuwa watuhumiwa wote watatu walikamatwa Juni 20, 2022 katika eneo la Hekcho lililopo kijiji cha Manolo wilayani Lushoto.
Kufuatia hukumu hiyo, Mwendesha Mashtaka wa TANAPA, Flavian Kalinga aliiomba Mahakama kuzitaifisha pikipiki hizo mbili ili liwe ni fundisho kwa watu wengine wanaojiusisha na makosa ya aina hiyo.

Akizungumza baada ya kutolewa hukumu hiyo mwendesha mashtaka Samwel Magoko (TANAPA),aliwaasa baadhi ya watu wenye nia ovu kuacha vitendo vya ujangili ili kuepuka mkono wa sheria. Hivyo wajishughulishe na kujipatia vipato kwa njia halali.
Na kuongeza vitendo hivyo vinarudisha nyuma juhudi za serikali za kuhifadhi na kulinda rasilimali hizo kwa faida ya kizazi cha sasa na cha baadae.