Na Munir Shemweta, JamhuriMedia, Katavi

Kamati ya Ushauri ya Maendeleo ya Mkoa wa Katavi (RCC) imependekeza Halmashauri ya Mpimbe kuwa wilaya kamili ambapo kwa sasa halmashauri hiyo iko katika wilaya ya Mlele.

Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi ambaye ni Mbunge wa Jimbo la Kavuu lililopo halmashauri ya Mpimbe wilaya ya Mlele ameshiriki kwenye kikao hicho kilichofanyika tarehe 20 Februari katika ofisi ya Mkuu wa mkoa wa Katavi.

Kikao hicho mbali na mambo mengine kilijadili na kupitisha Bajeti ya mkoa wa Katavi pamoja na Halmashauri zake kwa kipindi cha mwaka 2024/2025 sambamba na kupitia maeneo ya utawala.

Naibu Waziri wa Ardhi Mhe. Geophrey Pinda yuko mkoani Katavi ambapo mbali na shughuli nyingine atashiriki katika Mkutano Mkuu wa Jimbo la Kavuu kwenye halmashauri ya Mpimbwe mkoani Katavi.

Katika mkutano huo utakaofanyika Februari 24, 2024 katika Shule ya Sekondari Nizengo Pinda-Kibaoni Taarifa ya Utekelezaji wa Ilani ya CCM kuanzia Nov 2020 hadi Februari 2023 itawasilishwa na Naibu Waziri huyo.

Mgeni rasmi katika mkutano huo anatarajiwa kuwa Mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM na Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Kassim Majaliwa Majaliwa.

By Jamhuri