Na Helena Magabe, Jamuhuri Media Tarime.

Kulikuwa mvutano mrefu juu ya mgawayo wa pesa za CSR pale kiongozi mmoja aliyekuwepo Mara alipotaka pesa hizo zigawanywe kwenye wilaya nyingine nje Tarime.

Hali ilipelekea mgodi kusimama kwa muda kusubilia mvutano uishe hivyo ili uweze kutoa fedha hizo.

Hata hivyo hatimaye mvutano umeisha na mgawayo umekuwa kama ifuatavyo asilimia 70 ya pesa hizo itatumika katika vijiji vinavyozunguka mgodi.

Asilimia 30 itatumika katika vijiji vingine ambavyo viko nje ya mgodi vilivyopo Tarime Vijijini.

Mgodi umekuwa ukitekeleza wajibu wake kwa kutekeleza miradi inayobuniwa na madiwani na weyeviti wa vijiji.

Miaka ya nyuma kulikuwa na changamoto kubwa ya maji Nyamongo lakini kwa sasa wakazi hao wa Nyamongo wamepata maji ikiwa ni juhudi za viongozi.

Diwani wa Kata ya Matongo Godfley Kegoye amesimulia juu ya mradi wa maji pamoja na miradi mingine iliyotekelezwa kwa pesa za CSR.

Akianza na mradi wa maji anasema kata hiyo ina wakazi 34,900 sasa wananufaika na maji na hakuna tena kero ya maji Nyamongo.

Kata ya Matongo ina Vijiji vinne Mjini kati, Matongo, Nyabichune pamoja na Nyagoto ulipo mradi wa maji.

Kegoye anasema kabla hajaingia madarakani gari lilitumika kusambaza maji na katika Vijiji vinne na kusababisha foleni kubwa.

Amesema kwa sasa mgodi umejenga tanki kubwa la lita laki tatu (300,000)l enye uwezo wa kusambaza maji hata mkoa mzima wa Mara.

“Maji ni mengi sana yanaweza kusambazwa hata Mlmkoa mzima wa Mara ni masafi yanatoka mgodini na wao wanatumia hayo hayo kuna mtambo unayachuja uko mgodi harafu yaingia kwenye tenki” alisema Kegoye

Mradi huo wa maji wenye dhamani ya shilingi Milioni 9.98 zilizotumika kujenga tanki pia upo mtambo wa kuchuja maji hayo kutoka mgodini na kuyasafirisha kwenye hadi kwenye tank.

Mwenyekiti wa Kijiji cha Nyagoto Mwalimu Mwita Mossegi anasema kuanzia mwezi wa 6-8 kulikuwa na changamoto kubwa ya maji lakini maji mradi huo umewaokoa wananchi

Anasema kwa sasa asilimia kubwa ya wananchi wamevuta maji majumbani kwao kutoka kwenye tanki hilo.

Akiendelea kuzungumza anasema awali bili ya maji ilikuwa kubwa ambapo unit 1 ilighalimu shilingi 2000 baada ya malalamiko ya wananchi bei ilishushwa kwa sasa unit moja ni shilingi 1200.

Aidha anafafanua juu ya mchakato wa upatikanaji wa miradi kupitia pesa za CSR ambapo viongozi hubuni miradi na kupata ufadhili.

“Sisi tunakaa kikao cha WDC tunabuni mradi tunabuni mradi tunaupeleka Halmashauri Watalamu wanauchakata ukipewa ruhusa mgodi unatekeleza kuptia pesa za CSR” anasema Mossegi.

Mwenyekiti wa jumuiya ya maji, Dotto Mayeli Lino anasema kwa mujibu wa sensa ya mwaka 2022 wakazi wapatao 34,500 wananufaika na mradi huo wa maji.

Anasema wananchi wapatao 820 wamevuta mabomba majumbani kwao na wananchi 520 wamejaza fomu kwajili ya kuvuta maji hayo

Anasema mradi ulianza kutumika baada ya kuzinduliwa na Mwenge Julai 6,2023 na kuongeza kuwa kabla ya hapo kulikuwa na vituo viitwavyo DP ambayo vilitumika.

Akiendelea kuzungumza anasema kulingana na uwezo kutofautiana vituo hivyo vinaendelea kutumika ambapo kwa sasa foleni si changamoto tena.

Aidha Lino hakusita kuzungumza changamoto iliyokuwepo ya uchafuzi wa maji katika mto Tigite ambao ulichafuluwa na mgodi pamoja na mifugo.

Anaafanua kuwa kuna migodi miwili wa Nyarugusu pamoja na Nyabirama ambapo mgodi wa Nyarugusu ulichafua maji katika mto Tigite ambao unapita Kijiji cha Matongo.

Akiendelea kuzungumza amesema changamoto ya uchafuzi wa maji kupitia mgodi pamoja na mifugo ilipelekea watumiaji wa maji hayo kuugua maradhi ya tumbo mara kwa mara lakini kwa sasa hali ni nzuri baada ya kupatikana maji safi na salama

Mbali na hayo anasema ili kufanikisha zoezi la upatikanaji maji idara ya maji LUWASA ilishirikishwa hivyo mradi huo uko chini ya LUWASA.

Idara hiyo ya maji Tarime mjini na Tarime Vijijini ndiyo inayohusika na uwekaji mabomba pamoja na bill za maji.

By Jamhuri