Na Mwandishi Wetu, JamhuriMedia, Dodoma

Bohari ya Dawa (MSD),imedhamiria kujenga maghala matano ya kuhifadhi dawa na vifaa tiba katika mikoa mitano nchini.

Hayo yamebainisha leo Aprili 5,2023 na Mkurugenzi wa MSD, Mavere Tukai,wakati wa kikao kazi na wahariri wa vyombo mbalimbali vya habari kilichofanyika mkoani Dodoma.

Tukai amesema kuwa mpango mkakati walionao MSD ni kujenga maghala kwa lengo la kusogeza huduma karibu na wananchi.

Tukai ameelezea hivi sasa wapo mipango ya kufanikisha ujenzi wa maghala hayo kwa lengo la kuboresha utoaji huduma.

Mkurugenzi Mkuu wa Bohari ya Dawa (MSD) Mavere Tukai akizungumza leo Aprili 5,2023 jijini Dodoma wakati akifafanua mambo mbalimbali kuhusu Bohari ya Dawa kwenye semina ya siku mbili iliyoanza leo ambayo imeratibiwa na Bohari ya Dawa(MSD) kwa wahariri wa vyombo vya habari nchini.

“Tuna mpango wa kujenga maghala matano, tutajenga ghala kubwa Dar es Salaam, michoro tayari imekamilika na Dar es Salaam tunahudumia watu milioni 12.5, hivyo lazima tujenge ghala letu ambalo litakuwa kubwa.

“Pia tutajenga ghala Dodoma ambako ndiko kitovu kwa kuanza ambalo litahudumia Dodoma yenyewe, Singida na Tabora. Ghala lingine tutalijenga Mwanza ambako kule tunahudumia watu milioni 11. Tunakwenda kujenga ghala Mtwara.

“Katika Mkoa wa Kagera nako tunajenga ghala kwani kule hakuna ghala kabisa, tunahudumia kupitia Hospitali ya Muleba. Lengo la kujenga maghala kwenye mikoa hiyo tunataka kupunguza nguvu ya makao makuu. Tunataka huko kwenye kanda wawe na nguvu ya kuratibu na kuweka mipango yao wenyewe.”

Meneja Mawasiliano na Uhusiano Bohari ya Dawa (MSD) Eti Kusiluka akitoa maelekezo mafupi kabla ya kuanza kwa semina ya siku mbili ya  Wahariri wa Vyombo habari nchini leo  Aprili 5,2023 jijini Dodoma.

By Jamhuri