Na Mwandishi Wetu, JAMHURI MEDIA

Shirika la Reli Tanzania (TRC) limesitisha safari zake katika mikoa sita hapa nchini kutokana na mvua zinazoendelea kuonyesha katika maeneo mbalimbali.

Mikoa itakayoathiriwa na uamuzi huo wa TRC ni Dar es Salaam kuelekea mikoa ya Morogoro, Dodoma, Mwanza, Tabora, Mpanda na Kigoma.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa kwa Umma na kusainiwa na Meneja Uhusiano wa TRC, Jamila Mbaruk jana Machi 28,2023 uamuzi huo umefikiwa kutokana na mvua zinazoendelea kuonyesha maeneo mbalimbali nchini ambazo zimeathiri miundombinu.

“TRC imesitisha utoaji wa huduma kutokana na mvua kubwa zinazoendelea kunyesha maeneo mbalimbali na kusababisha daraja kusombwa na maji kati ya stesheni ya Godegode na Gulwe, Wilaya ya Mpwapwa mkoani Dodoma,” imeeleza taarifa hiyo.



Kufuatia adha hiyo TRC imesema huduma za usafiri zitarejea Machi 30 huku ikiwaomba wananchi radhi kwa usumbufu huo na kuwahakikishia kwamba usafiri huo utarejeshwa.

Hata hivyo, kwa kipindi kirefu eneo la Godegode limekuwa ni korofi katika msimu wa mvua na kusababisha mara kadhia treni kusitisha safari zake kutokana na maji yanayoshuka kutoka milima ya Kibakwe kuharibu miundombinu.

Itakumbukwa Januari, 2020 TRC ilisitisha uuzwaji wa tiketi mkoani Dodoma kutokana na eneo la Godegode – Gulwe mkoani humo kutoruhusu treni kupita.

By Jamhuri