Na Mwandishi Wetu, JamhuriMedia, Morogoro

Mkuu wa Mkoa wa Morogoro Fatma Mwassa amewataka wakazi wa mkoa huo kuwa walinzi na kuheshimu mipaka ya hifadhi ya vyanzo vya maji na kwamba serikali itawachukulia hatua kali za kisheria wale wote watakao husika na vitendo vya kuchoma moto hifadhi ya vyanzo vya maji ikiwemo kuwafikisha mahakamani kwa mujibu wa sheria.

Ametoa agizo hilo wakati wa uzinduzi wa kampeni ya kupanda miti rafiki ya maji inayotekelezwa na Bodi ya maji Bonde la Wami Ruvu ambapo amesema atakayebainika kujihususisha kwa namna yeyote na vitendo vya uharibifu wa mazingira kwa kuchoma moto au kufanya shughuli nyingine za kibanaadamu atachukuliwa hatua ikiwemo kifungo cha miaka saba gerezani.

Amesema katika kuhakikisha eneo linabaki katika uhifadhi tayari mamlaka zimekabidhi jukumu la ulinzi kwa kikosi maalumu cha jeshi la wananchi kwa kushirikiana na jeshi la akiba ambao watakuwepo eneo hilo kwa saa 24.

“Sasa hivi bwawa hili linalindwa na kikosi maalumu cha Jeshi la Wananchi wakishirikiana na Jeshi la Akiba kwa saa 24, sasa mtu yeyote uje ufanye fujo zako utaangukia kwenye sheria, ukijenga kibanda au kuchoma moto utasahaulikia jela miaka 7” amesema Mkuu wa Mkoa.

Aidha amewataka wale wote wanaofanya shughuli za kibinaadamu karibu na bwawa hilo kuacha kabisa kwani atakayebainika kufanya hivyo hatua za kisheria zitachukuliwa juu yake kwa mujibu wa sheria ya mazingira.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Bodi ya maji Bonde la Wami Ruvu Elibarik Mmassy amesema kampeni hiyo inalenga kupanda miti milioni 2 katika maeneo mbalimba ya vyonzo vya maji katika Mkoa wa Morogoro.

Amesema kwa sasa bwawa la mindu linakabiliwa na changamoto ya tope lililochangiwa na shughuli za kibinaadamu kandokando ya bwawa hilo ikiwemo uchumoji wa miti kwajili ya uandaaji wa mashamba hali iliyochangia kupungua kwa kina cha maji na kuathiri upatikanaji wa maji katika mji wa Morogoro.

By Jamhuri