………………………………………………………………………..

Waziri wa Katiba na Sheria nchini Dkt. Damas Ndumbaro amefanya ziara ya kikazi mkoani Shinyanga kwa lengo la kukagua utekelezaji wa kampeni ya huduma ya msaada wa kisheria inayojulikana kwa jina la Mama Samia legal Aid Campaign.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo leo Juni 15, 2023, Waziri wa Katiba na Sheria nchini Dkt. Damas Ndumbaro ameupongeza Mkoa wa Shinyanga kwa kufanya vizuri kwenye kampeni hiyo Mama Samia legal Aid Campaign na kusema kuwa kampeni hiyo itapita kwenye kila kijiji na kumaliza changamoto zilizokuwa zinawakabili wananchi wanyonge kwa kutofahamu sheria.

“Kampeni hii ambayo imepewa heshima kubwa kwa kupewa jina la kiongozi wetu mkuu wa nchi inatokana na Ilani ya Chama Cha Mapinduzi ambayo imeagiza waananchi wapate elimu ya sheria na msaada wa sheria katika kutatua changamoto mbalimbali wanazozikabili, lakini pia kampeni hii ni maelekezo ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ndipo wizara ikaja na kampeni hii hivyo niwapongeze Mkoa wa Shinyanga kwa kuendelea kutoa huduma ya msaada wa kisheria ”, amesema Waziri Ndumbaro.

“Lengo mahususi la kampeni hii ni kuhakikisha kuwa kuna haki, amani, usawa na maendeleo katika nchi, programu yetu itawafikia nchi nzima bara na visiwa na niwahakikishie kuwa watendaji wabovu hakuna namna tutawachomoa, watendaji ambao kazi yao ni kudhulumu haki za wananchi hatutawaacha salama na tutaanza na mkoa huu wa Shinyanga”, ameongeza Waziri Ndumbaro.

Aidha Waziri Damas Ndumbaro ametatua mgogoro wa kifamilia uliodumu kwa miaka nane katika kijiji cha Wishiteleja kata ya Mondo wilayani Kishapu mkoani humo na kufanya mkutano wa hadhara na wananchi wa kata ya Maganzo ambapo kupitia mkutano huo ametoa elimu na kusikiliza migogoro iliyokuwa ikiwakabili wakazi wa eneo hilo.

Awali akitoa taarifa ya utekelezaji wa Kampeni ya Mama Samia legal Aid Campaign ngazi ya mkoa, Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga Mhe. Christina Mndeme amesema kampeni hiyo imekuwa msaada mkubwa katika kutatua migogoro ya iliyokuwa ikitokana na ukosefu wa elimu ya masuala ya sheria na kusema miongoni mwa sababu zinazopelekea migogoro ni tabia ya baadhi ya watumishi kukosa maadili ya misingi na taratibu ya kazi yao.

“Mara baada ya kuanzishwa kwa kampeni hii ya msaada wa kisheria imekuwa ni mkombozi mkubwa kwenye jamii kwa kupunguza migogoro ya ardhi, urithi na mambo mengine yanayohusiana na sheria. Kupitia kampeni hii dhuruma waliokuwa wakikumbana nayo wananchi na kukosa haki zao sasa inakwenda kuisha kwani mpaka sasa malalamiko yamepungua. Tunamshukuru sana Mheshimiwa Waziri kwa kutuletea kampeni hii ndani ya mkoa tunaahidi kuendelea kutoa ushirikiano ili malengo ambayo serikali imejiwekea yaweze kufikiwa”, amesema RC Mndeme.

Pia Mndeme amemuomba Waziri wa Katiba na Sheria kupitia upya vifungu vya sheria vinavyotoa dhamana kwa wanaokutwa na hatia ya kujihusisha na vitendo vya ubakaji na ulawiti kwani imekuwa chanzo cha kujirudia kwa matukio ya vitendo hivyo.

Waziri wa Katiba na Sheria nchini Dkt. Damas Ndumbaro kulia akipeana mkono na Limi Jokala mara baada ya kusuluhisha mgogoro uliokuwa ukimsumbua kwa muda mrefu.

Waziri wa Katiba na Sheria nchini Dkt. Damas Ndumbaro akizungumza na wananchi wa kata ya Maganzo.

Mkazi wa kata ya Maganzo Nyale Numbu akizungumza wakati wa mkutano wa Hadhara.
Mkazi wa kata ya Maganzo Juma Kapina akizungumza wakati wa mkutano

By Jamhuri