Na Mwandishi Wetu, JamhuriMedia

Benki ya NMB imeahidi kutoa bidhaa zinazokidhi mahitaji ya wanadiaspora ilikuwawezesha kushiriki kikamilifu katika shughuli za ujenzi wa Taifa.

Hayo yalisemwa na Afisa Mkuu wa Wateja Binafsi na Biashara Benki ya NMB Filbert Mponzi wakati akihudhuria hafla ya uzinduzi rasmi wa Mfumo wa kuwasajili Diaspora wenye asili ya Tanzania Kidigitali yaani Diaspora Digital Hub jana ulioanzishwa na Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki ambao pamoja na mambo mengine unalenga kuanzisha kanzi data ya waTanzania wote walioko ughaibuni.

Mponzi alisema Benki ya NMB inatambua kuwa wanadiaspora wana mchango mkubwa katika mchakato wa maendeleo ya nchi na kuongeza kuwa benki hiyo itaendelea kuwekeza kwenye mifumo ya kuwawezesha Watanzania walioko ughaibuni kupata bidhaa na masuluhisho ya kibenki kama sehemu ya dhamira yake ya kuongeza mchango wao katika ujenzi wa Taifa.

“Kama benki, tulitia saini Mkataba wa Makubaliano (MoU) na Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki na kutoa shilingi milioni 100 mwezi Agosti mwaka jana kusaidia uanzishwaji wa Mfumo wa kuwasajili Diaspora wenye asili ya Tanzania Kidigitali na tunafurahi kuona mfumo huu upo tayari kuzinduliwa leo. Tunaamini kuwa mfumo huu utasaidia katika kuongeza mchango wa wanadiaspora katika mchakato wa maendeleo ya uchumi wa nchi,” Mponzi alisema.

Alibainisha kuwa katika dhamira yake ya kutoa huduma za kipekee za kibenki kwa wanadiaspora, benki yake ilianzisha idara maalumu kwa ajili ya kuhudumia masilahi ya Watanzania wanaoishi ughaibuni.

Awali Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Samweli Shelukindo wakati wa hafla hiyo alisema mfumo huo si tu utasaidia kufuatilia taarifa zote muhimu kwa Watanzania walioko ughaibuni bali pia utasaidia katika kuwaunganisha na huduma mbalimbali hapa Tanzania kama vile huduma za benki na fedha, huduma za Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (NIDA) na Wakala wa Usajili Ufilisi na Udhamini (RITA).

“Ni dhahiri kuwa mfumo huu utasaidia Watanzania walioko ughaibuni kujua fursa za uwekezaji zilizopo nyumbani,” alisisitiza.

Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama Vita Kawawa alibainisha kuwa uzinduzi wa mfumo huo ni, “hatua muhimu na ni mwelekeo sahihi katika kuimarisha mchango wa diaspora katika maendeleo ya nchi”.

Naye Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Dkt. Stergomena Tax wakati wa hafla hiyo alisema mchango wa wanadiaspora umekuwa ukiongezeka katika miaka ya hivi karibuni na kubainisha kuwa kati ya Januari hadi Desemba 2021, Watanzania wanaoishi nje ya nchi walituma takribani dola za Marekani milioni 569.3 nyumbani.

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Dk. Stergomena Tax
(kulia), akimkabidhi cheti cha shukrani Afisa Mkuu wa wateja Binafsi na Biashara wa
Benki ya NMB, Filbert Mponzi (kushoto), wakati wa hafla ya uzinduzi wa mfumo wa
kukusanya na kutunza taarifa za Diaspora Kidigitali (DDH) ambapo Benki ya NMB
imefadhili utayarishaji wa mfumo huo. (Na Mpiga Picha Wetu).

“Kati ya Januari hadi Desemba 2022, Watanzania wanaoishi ughaibuni walituma dola za Marekani bilioni 1.1 (takriban 2.6trn/-. Hizi si fedha kidogo. Tunaelewa kuwa baadhi ya watu wanaoishi ughaibuni hawatumii njia rasmi kutuma hela nyumbani. Tunafurahi kwamba mfumo huu tunaozindua leo unajumuisha taasisi za kifedha kama Benki ya NMB ili kuziba pengo hili,” aliongeza.

Alibainisha kuwa mchango wa diaspora katika sekta ya ardhi na nyumba mwaka jana ulifikia dola milioni 4.4 kutoka milioni 2.3 mwaka 2021.
“Watanzania wanaoishi ughaibuni pia waliwekeza takribani shilingi 2.5 katika Dhamana ya Uwekezaji Tanzania (UTT),” aliongeza.

Alibainisha kuwa Wizara hiyo kwa miaka mingi haikuwa na kanzi data ya pamoja kwa ajili ya Watanzania wote walioko ughaibuni hali iliyozifanya balozi mbalimbali za Tanzania nje ya Tanzania kuja na kanzi data tofauti kwa ajili ya Watanzania wanaoishi nje ya nchi.

“Kila ubalozi siku za nyuma ulikuwa na kanzi data yake na hii ilikuwa changamoto katika utoaji wa huduma. Kama wizara, tuliona haja ya kuwa na Mfumo wa kuwasajili Diaspora wenye asili ya Tanzania Kidigitali na tunafurahi kwamba mfumo huu sasa upo tayari kuzinduliwa leo,” Dk. Tax alisema.

Dkt. Tax wakati wa hafla hiyo alitoa changamoto kwa watendaji wa wizara yake kuhakikisha wanaunganisha Mfumo wa Dijitali wa Diaspora na mifumo mingine ya Serikali ili kuongeza ufanisi na utoaji wa huduma.

Dkt.Tax wakati wa hafla hiyo alitoa changamoto kwa watendaji wa wizara yake kuhakikisha wanaunganisha Mfumo wa kuwasajili Diaspora wenye asili ya Tanzania Kidigitali na mifumo mingine ya Serikali ili kuongeza ufanisi na utoaji wa huduma.

“Hii inapaswa kwenda sambamba na kampeni ya kujenga uelewa kwa umma ili kuhakikisha kwamba watu wanaoishi nje ya nchi wanapata taarifa zote muhimu zinazohitajika,” alisema.

By Jamhuri