Jumla ya shilingi milioni 170 zimetolewa katika mkupuo wa kwanza ambapo msanii wa chini amepata shilingi milioni 20 na wa juu amekopeshwa kiasi cha shilingi milioni 50.

Akikabidhi hundi hizo Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo,Mohamed Mchengerwa amewataka wasanii na wadau wa kazi za sanaa kujitokeza kwa wingi kuomba kukopeshwa fedha kutoka kwenye mfuko huo alioufufua Rais wa Jamhuri ya Muungano,Samia Suluhu Hassan kwa lengo la kuwakwamua kiuchumi.

Amesema kuwa hundi za mamilioni ya fedha zimetolewa kwa wadau waliokidhi kukopa kwenye mfuko wa Utamaduni na Sanaa kwani awali mfuko huo haukuwepo tangu mwaka 2013 ulipositishwa ule wa awali.

Mchengerwa amesema hayo jana jijini Dar es Salaam akiwa na Katibu Mkuu wa Wizara hiyo Dkt. Hassan Abbasi kwenye uzinduzi rasmi wa utoaji mikopo kutoka kwenye mfuko huo ambapo uzinduzi huo pia ulihudhuriwa na viongozi na wadau mbalimbali wa Sanaa na Utamaduni.

Aidha, wakati wa uzinduzi huo wadau wa tano kati ya kumi na tisa waliowasilisha maombi yao walipatiwa fedha za mfuko huo.

By Jamhuri