Na Mary Margwe, JamhuriMedia, Hanang

Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga Christina Mndeme amekabidhi misaada ya kibinadamu ikiwemo vyakula, nguo na vifaa vya ujenzi vilivyotolewa na wananchi wa Shinyanga kwa waathirika wa mafuriko ya tope yaliyoambatana na mawe kutoka mlima Hanang’ katika Wilaya ya Hanang’ Mkoani Manyara.

Akikabidhi msaada huo kwa Mkuu wa Wilaya ya Hanang Janeth Mayanja, huku Mndeme akiwa ameambatana na Mkuu wa Wilaya ya Shinyanga Bi.Johari Samizi na Mkuu wa Wilaya ya Kahama Bi. Mboni Mhita.

Mndeme amesema Wana Shinyanga wanaungana na Mhe. Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan kutoa pole kutokana na janga lililotokea Hanang lililosababishwa mvua kubwa iliyoambana na tope, mawe na miti hivyo kupelekea vifo, mali kupotea, mifugo kufa, mashamba kuharibika, nyumba kuharibika na zingine kusambaratika kabisa.

“Kufuatia hilo, kwakua wana Shinyanga ni miongoni mwa sehemu ya Watanzania tulioguswa sana na janga hili na tulipokea tatizo hili kwa masikitiko makubwa, baada ya kupokea taarifa hii ya kusikitisha, wanashinyanga kwa mapenzi mema wakaona nao ni vema wamuunge mkono Rais Samia Suluhu Hassan lakini vile vile waungane na wananchi nwengine kutoa pole kwa wananchi wa Hanang hivyo tumefika hapa katika mji huu wa Katesh kuwasilisha kwako mhe. DC Janeth Mayanja pole zetu ili kuonesha mshikamano, umoja na kwamba tuko pamoja katika kipindi hiki kigumu ambapo kwa wenzetu wa Hanang’ wanapitia”,amesema Mkuu wa Mkoa Mndeme.

Aidha Mndeme amebainisha miongoni mwa vitu vilivyotolewa kuwa ni pamoja na mifuko 1000 ya saruji, Mchele kilo 700, unga wa Mahindi kilo 355, unga lishe kilo 25, juice katoni 500, chumvi pakti 90, sukari kilo 25, sabuni katoni 13, mafuta ya kula Lita 5, viatu pea 43, nguo balo 30 ambapo kati ya hizo balo 27 za wanaume, na balo 3 ni nguo mchanganyiko.

“Kwa niaba ya wananchi wa Shinyanga ambao wamejitolea kutoa pole zao kwa ndugu zao wa Hanang, naomba nikakibidhi mifuko 1000 ya saruji, mchele kilo 700, unga wa mahindi kilo 355, unga lishe kilo 250,juisi katoni 500, chumvi pakti 90,sukari kilo 25, sabuni katoni 13,mafuta ya kula lita 5, viatu pea 43, nguo balo 30 kati ya balo hizo 27 zina nguo za wanaume na tatu nguo mchanganyiko” amesema Mndeme.

Ameongeza kuwa misaada hiyo inatoka kwa wananchi wa Mkoa wa Shinyanga, waliojitoa Kwa mapenzi yao mema,ambapo wameguswa nanhatimaye wameweza kuchangia vitu hivyo.

“Misaada hii inatoka kwa wananchi wa mkoa wa Shinyanga ambao wamejitolea kwa mapenzi yao mema, wameguswa kwa namna moja au nyingine. Poleni sana wan Hanang, pole sana Mhe. Rais Samia, tuendelee kumuomba Mungu atuepushe na majanga haya, mvua tunaihitaji, tunaumuomba Mungu atuletee mvua yenye neema. Msaada tuliotoa ni mdogo ukilinganisha na madhara yaliyotokea tunaomba hiki kilichotolewa na wana Shinyanga mkipokee”,ameongeza Mndeme.

Akipokea misaada hiyo, Mkuu wa Wilaya ya Hanang Janeth Mayanja amewashukuru Mkuu wa Mkoa huyo pamoja na Wana Shinyanga kwa ujumla kwa upendo,huruma, utu, ubinadamu na undugu wa kweli waliouonesha kwa wana Hanang ambapo amesema kufanya hivyo ni kuunga mkono jitihada za Mh. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Mkuu huyo wa Wilaya pia amesema kitendo hiko ni Cha kiungwana ambacho kitawafariji waathirika nankuwatia Moyo katika mapito waliyopitia, hivyo kwanujumpa Wana Hanang wana washukuru sana.

“Tunawashukuru sana Wana Shinyanga kwa misaada ya kibinadamu mliyotupatia, mmeongeza nguvu Hanang na vifaa hivi vya ujenzi mlivyotoa vitasaidia katika ujenzi wa makazi ya waathirika wa janga lililotokea” amesema.

By Jamhuri