Safari ya elimu Tanzania

Katika dunia ya leo, ili kila mtu aweze kuboresha maisha yake ni lazima awe na elimu. Elimu ndiyo inayomwezesha mtu kujitambua na kujimiliki yeye mwenyewe kwanza, pia kuzikabili changamoto zinazomsonga, kuyatawala na kuyatumia mazingira yanayomzunguka ili kuboresha maisha yake.

Ndani ya utandawazi, elimu isiyotosheleza tafsiri yake ni umaskini zaidi; wakati elimu zaidi tafsiri yake ni maisha bora zaidi.

Nelson Mandela, Rais mstaafu wa Afrika Kusini, amewahi kusisitiza umuhimu wa elimu kwa maendeleo ya jamii, kwa kusema kuwa:  “elimu ni injini kubwa ya maendeleo ya mtu. Ni kupitia elimu ndipo binti wa mkulima mdogo anaweza kuwa daktari bingwa, kwamba mtoto wa kibarua wa mgodini anakuwa mkuu wa mgodi, na mtoto wa kibarua wa mashambani anakuwa rais wa taifa kubwa.”

Ili elimu iweze kuleta mabadiliko ya kweli kimaendeleo, ni lazima iwe elimu bora ambayo inalenga kumbadilisha mtu na kumwezesha kufikiri, kubuni, kujitambua, kuhoji, kudadisi, kupenda kazi, kuwa na mwenendo mwema na kuboresha afya na maisha yake binafsi na ya jamii. 

Elimu ni ukombozi iwapo italenga kumpatia mtu uwezo wa kupambana na changamoto zinazoikabili jamii na taifa kwa ujumla. Elimu inamjenga mtu kuwa raia makini na mzalishaji ndani ya nchi yake.

Historia ya elimu nchini inatukumbusha malengo ya msingi ya elimu Tanzania. Ukiacha elimu ya kibaguzi iliyokuwa inatolewa kabla ya uhuru, elimu ya Tanzania baada ya uhuru ililenga kumjenga mtu katika nyanja zote ili awe mzalishaji mzuri katika nchi yake.

Ndiyo maana elimu na kazi vilisisitizwa, na vyuo vya ufundi pamoja na kazi za mikono vilipewa msisitizo mkubwa, huku suala la usawa, haki na misingi ya umoja wa kitaifa vikichanua na kushamiri kwenye nyaraka za serikali na kwenye vichwa vya watu.

Dhamira hii ikaleta maboresho makubwa yakiwamo ongezeko kubwa la uandikishaji, kutaifishwa kwa shule za binafsi na kufanywa za umma na kuzaliwa kwa Azimio la Arusha lililokuja kuwa dira ya kusimamia misingi ya haki, usawa, udugu na utu.

Solomon Eliufoo ndiye aliyeongoza michakato hii kama Waziri wa Elimu kutoka mwaka 1962 hadi 1965.

Katika kipindi chake, Eliufoo alipiga marufuku ada kwa wanafunzi wa sekondari, kuendeleza ujenzi wa shule za msingi na sekondari na upanuzi wa mafunzo kwa walimu wa daraja A na C na elimu ya watu wazima.

Pia ndani ya miaka hii mabadiliko mengine tuliyoshuhudia ni kuruhusiwa kwa Kiswahili kutumika kama lugha ya kufundishia katika elimu ya msingi na Kiingereza kwas sekondari, kupinga ubaguzi wa rangi katika elimu na elimu ya msingi kutangazwa kutolewa kwa miaka minane.

Kipindi cha 1965 hadi 1970 chini ya Waziri Chediel Mgonja, kilishuhudia uamuzi wa Rais wa Awamu ya Kwanza, Julius Kambarage Nyerere, akitangaza rasmi falsafa mpya ya elimu iliyojulikana kwa jina la Elimu ya Kujitegemea, kuanzishwa kwa Taasisi ya Elimu na uundwaji wa Baraza la Mitihani la Afrika Mashariki.

Mabadiliko mengine katika kipindi hiki yalihusu kutungwa kwa Sheria ya Elimu ya mwaka 1969, shule za msingi kufundishwa na Watanzania pekee na kuimarishwa kwa kisomo cha watu wazima na chenye manufaa.

Elimu ya watu wazima ndiyo iliyojenga nchi na kuiweka kwenye hadhi ya juu katika medani za kimataifa, hasa kwenye suala la upunguzaji wa ujinga.

Hadi kufikia mwaka 1986 kiwango cha Watanzania kujua kusoma na kuandika kilikuwa ni asilimia 91, tofauti na sasa ambapo kimeshuka hadi asilimia 69 kwa mujibu wa utafiti uliofanywa na Taasisi ya HakiEilmu mwaka 2001 na 2010. Miaka ya 1975 hadi 1980 ilishuhudia mabadiliko mengi tu kwenye mfumo wa elimu yetu.

Ni kati ya miaka hiyo, ujenzi wa vyuo vya maendeleo ya wananchi ulifanyika, kutolewa kwa Tamko la Elimu ya Msingi kwa wote, ujenzi wa vituo vya ufundi kwa wahitimu wa elimu ya msingi na kuzuiwa kwa mtihani wa darasa la nne. 

Pia Taasisi ya Ukuzaji Mitaala na Taasisi ya Elimu ya Watu Wazima vilianzishwa. Na mwaka 1978 ndiyo kipindi ilipotungwa Sheria ya Elimu namba 25 chini ya Waziri Nicholas Kuhanga.

Kuanzia mwaka 1995 hadi 2005, mengi yamefanyika ikiwamo kuanza kwa Programu ya Maendeleo ya Sekta ya Elimu (ESDP), kuanza kwa Mpango wa Maendeleo wa Elimu ya Msingi (MMEM) na Mpango wa Maendeleo wa Elimu ya Sekondari (MMES).

Mipango hii ndiyo inayoshika hatamu za kuiendesha elimu yetu kuelekea kwenye ubora na fursa sawa kwa wote. Je, tija ya mabadiliko haya tangu uhuru ina mwelekeo  gani kwa Taifa? Dira ya Maendeleo ya Taifa 2025, Mkakati  wa Kukuza Uchumi na Kupunguza Umaskini (MKUKUTA), Mpango wa Maendeleo ya Elimu ya Msingi (MMEM), Mpango wa Maendeleo.

Taarifa ya idadi ya watu wasiojua kusoma na kuandika aliyoitoa Naibu Waziri wa Elimu, Philip Mulugo bungeni Februari 15, 2011 ya Elimu ya Sekondari (MMMES) na Sera ya Elimu na Mafunzo vyote vinabainisha ukweli huu kuwa ili Tanzania ipige hatua kali za kimaendeleo ni lazima wananchi wake wapate elimu bora iliyokamilika. 

Lakini  je, elimu inayotolewa hapa Tanzania inakidhi haya yote? Ama ni kwa kiasi gani inawawezesha watoto na vijana kufikia malengo hayo? Hili ndilo swali la msingi linalopaswa kutuongoza kuelekea kwenye mipango na vitendo vinavyoipeleka mbele elimu yetu na siyo kuirudisha nyuma.

Hivi karibuni tumesikia mengi kutoka kwa viongozi wetu kuhusu elimu hapa nchini akiwamo Rais wa Awamu ya Tano, Dk. John Pombe Magufuli, akisemea kutoa elimu bure kwa watoto kuanzia awali hadi kidato cha nne.

Watanzania wanapenda elimu yenye ubora na siyo tu kwa kuwa itatolewa bure iwe chini ya kiwango, tunaamini kuwa “vya bure havina thamani” lakini hatutarajii kuona upuuzi huu ukiendelea. 

Imekuwa kawaida kuwaona wanafunzi waliohitimu darasa la saba wakiwa hawajui kusoma na kuandika. Masikio ya Watanzania na macho wanatamani kuiona kauli ya “elimu bure” ikifanyiwa utekelezaji mapema Januari mwaka ujao.  

Hadi mwaka 2010 zaidi ya watoto milioni 8 (ambao ni zaidi ya asilimia 90 ya uandikishaji halisi) wameandikishwa shule za msingi na zaidi ya wanafunzi 1,638,699 wako sekondari.

 

 [email protected]