• Asema ziara yake Urusi imefungua milango, imelinda sera ya Tanzania
  • Nchi sasa iko tayari kupokea wawekezaji kutoka Marekani, Ulaya
  • Wapewa hekta 6,000 Morogoro kulima ndizi, watalii kuanza Julai
  • Shirika la Nishati ya Nyuklia la Serikali ya Urusi – ROSATOM kusaidia

Na Deodatus Balile, Moscow, Urusi

Ziara ya Rais Samia Suluhu Hassan nchini Urusi imefungua milango mipya ya uwekezaji, biashara, elimu na teknolojia huku ikiimarisha sera ya Tanzania ya kutofungamana na upande wowote, JAMHURI limebaini.

Akizungumza na waandishi wa habari jijini St. Petersburg, Rais Samia amesema Urusi imeifungulia milango Tanzania na imejipanga kuja kufanya uwekezaji katika madini, kilimo, usafirishaji, elimu na maeneo mengi yatakayowanufaisha vijana wa Kitanzania.

Kutokana na kupita miaka 57 bila wakuu wa nchi hizi mbili kutembeleana, Rais Samia amesema: “Yaani tulipofika, ilikuwa tunaulizana, mwezangu ulipotelea wapi muda wote huu… kwa kweli ziara imefana sana. Tumepewa mapokezi ya heshima kubwa sana.”

Kati ya matokeo ya moja kwa moja ya ziara hiyo, Tanzania imeipa Urusi hekta 6,000 mkoani Morogoro ambapo watalima ndizi na kuuza nchini Urusi. Ndege za Air Tanzania na Shirika la Ndege la Urusi nazo zitaanza kufanya safari zake, huku mradi wa urani wa Mto Mkuju mkoani Ruvuma ukiendelea kwa kasi.

Ziara ya kiserikali ya Rais Samia nchini Urusi kuanzia Juni 3 hadi 5, 2026, imeelezwa na wengi kuwa moja ya ziara zenye uzito mkubwa zaidi wa kidiplomasia katika historia ya karibuni ya Tanzania. Zaidi ya safari ya kawaida ya kikazi nje ya nchi, ziara hii imetafsiriwa kama marekebisho ya kimkakati ya uhusiano wa nchi hizi mbili, ikiuhuisha ushirikiano ambao ulikuwa umelegalega kwa zaidi ya nusu karne tangu ziara ya kihistoria ya Mwalimu Julius Nyerere mwaka 1969.

Kiini cha ziara hiyo kilikuwa mkutano wa ngazi ya juu kati ya Rais Samia na Rais wa Urusi, Vladimir Putin, katika Ikulu ya Kremlin. Mazungumzo yao hayakuwa ya kiitifaki tu, bali yalijikita kwa kina katika masuala ya mabadiliko ya kiuchumi, usalama wa nishati, ushirikiano wa viwanda, elimu na mwelekeo wa kijiopolitiki ndani ya mfumo wa sera ya muda mrefu ya Tanzania ya kutofungamana na upande wowote.

Moja ya viashiria vya wazi vya mafanikio ya ziara hiyo ni ukubwa wa ahadi za kiuchumi na mazungumzo yanayoendelea ambayo yalithibitishwa upya au kupanuliwa. Tanzania imejipambanua kuwa nchi tulivu, yenye mageuzi na inayofaa kwa uwekezaji, huku Urusi ikionyesha nia thabiti katika sekta za kimkakati.

Mradi mkubwa unaobeba ushirikiano huo ni Mradi wa Urani wa Mto Mkuju, mkoani Ruvuma, ambapo uwekezaji unaoungwa mkono na Urusi wenye thamani ya takribani Dola za Marekani bilioni 1.2, zaidi ya Sh trilioni 3, tayari uko katika hatua ya utekelezaji kupitia Mantra Tanzania Limited, kampuni tanzu ya Shirika la Nishati ya Nyuklia la Serikali ya Urusi (ROSATOM).

Mradi huo peke yake unatarajiwa kubadilisha mfumo wa uchimbaji madini na viwanda vinavyohusiana na nishati nchini Tanzania.

Kwa mujibu wa makadirio yaliyojadiliwa wakati wa ziara hiyo, mradi huo unaweza kuzalisha takribani tani 3,000 za urani kwa mwaka na kuingiza mapato baada ya mauzo ya nje yanayokadiriwa kufikia Dola milioni 4 kwa mwaka kama gawio.

Zaidi ya mapato hayo, unatarajiwa kuajiri hadi vijana 20,000 wa Kitanzania, jambo linaloufanya kuwa moja ya miradi mikubwa zaidi ya ajira za moja kwa moja katika sekta ya uchimbaji nchini katika historia ya hivi karibuni.

Ahadi kubwa zaidi iliyotokana na ziara hiyo ni ushirikiano katika maendeleo ya nishati ya nyuklia. Tanzania na Urusi zilikubaliana kuangalia uwezekano wa kujenga mtambo wa kwanza wa umeme wa nyuklia nchini Tanzania wenye uwezo wa kuzalisha hadi megawati 100 mkoani Pwani, ambapo inatarajiwa kinu cha kwanza cha kuzalisha umeme kuwa tayari mwaka 2029.

Mradi huo, utakaotekelezwa kwa ushirikiano na ROSATOM, unawakilisha mabadiliko makubwa katika mkakati wa muda mrefu wa nishati wa Tanzania. Mtambo huo unatarajiwa kuongeza uhakika wa upatikanaji wa umeme, kusaidia ukuaji wa viwanda na kupunguza utegemezi wa umeme wa maji ambao huathiriwa na mabadiliko ya tabianchi.

Rais Samia amesema mtambo huo ni mwanzo wa safari ya Tanzania kufikisha megawati 8,000 mwaka 2030 na megawati 70,000 mwaka 2050, muda ambao Tanzania itakuwa na uchumi wa Dola trilioni moja kwa mujibu wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

Wakati huo Tanzania itakuwa nchi ya viwanda na moja ya nchi zenye uchumi mkubwa zaidi barani Afrika.

Kwa Tanzania, huu si mradi wa nishati tu, bali ni hatua ya maendeleo ya kimkakati. Upatikanaji wa umeme wa uhakika na wa kiwango kikubwa unachukuliwa kuwa msingi wa ukuaji wa viwanda, mageuzi ya kidijitali na uzalishaji wa ajira kwa kiwango kikubwa.

Ujumbe kutoka kwa utawala wa Rais Samia uko wazi kwamba usalama wa nishati ni msingi wa mageuzi ya kiuchumi.

Zaidi ya nishati ya nyuklia, Urusi imeonyesha utayari wa kupanua ushirikiano katika gesi asilia, gesi kimiminika (LNG), umeme wa maji pamoja na teknolojia za nishati. Majadiliano hayo yanaendana kwa karibu na azma ya Tanzania ya kuwa taifa la viwanda linaloendeshwa na nishati ya uhakika yenye mseto.

Athari yake ni uwezekano wa ushirikiano wa kina unaojumuisha uchimbaji, usindikaji, maendeleo ya miundombinu na uhamishaji wa teknolojia. Ikiwa utatekelezwa kikamilifu, unaweza kupunguza kwa kiasi kikubwa pengo la ufadhili wa miundombinu nchini Tanzania na kuongeza kasi ya uzalishaji viwandani.

Matokeo mengine muhimu ya ziara hiyo ni kuimarika kwa ushirikiano katika elimu na utafiti wa kisayansi. Rais Samia ametunukiwa Shahada ya Heshima na Chuo Kikuu cha Urafiki wa Watu wa Urusi (RUDN), ikiwa ishara ya kuongezeka kwa uhusiano wa kitaaluma kati ya nchi hizi mbili.

Mkuu wa Chuo cha RUDN, Oleg Yastrebov, amesema chuo hicho kilichoanzishwa mwaka 1960 kwa sasa kina wanafunzi wa kimataifa 13,000. Ameongeza kuwa tangu kuanzishwa kwake, Watanzania 1,132 wamesoma chuoni hapo.

Tanzania inashika nafasi ya pili kwa wingi wa wanafunzi waliosoma chuoni hapo, ikitanguliwa na Nigeria ambayo wanafunzi wake 1,515 wamewahi kusomea katika chuo hicho.

Rais Samia, wakati akipokea shahada hiyo, amesema: “Elimu na uhuru havitenganishwi. Vyuo vikuu vinatoa ukombozi na maendeleo kwa binadamu kwa maendeleo endelevu.”

Ameongeza kuwa idadi ya Watanzania wanaosoma Urusi itaongezeka baada ya kuanzishwa kwa mpango wa Samia Scholarship unaotoa nafasi kwa wanafunzi bora kusoma masomo ya sayansi, teknolojia na uhandisi.

Amesisitiza kuwa maarifa yanakuwa na maana pale yanapohudumia jamii.

Mazungumzo pia yalijikita katika kuongeza ufadhili wa masomo kutoka wanafunzi 150 kwa mwaka kwa sasa hadi 250, huku miradi ya pamoja ya utafiti na ushirikiano wa taasisi katika sayansi, teknolojia, uhandisi na ubunifu ikiandaliwa.

Lengo ni kujenga mtaji wa rasilimali watu, ambao ni nguzo muhimu ya ajenda ya Tanzania ya viwanda.

Lengo pana ni kuhakikisha Tanzania haipokei mitaji ya uwekezaji pekee, bali pia maarifa, teknolojia, ujuzi wa kiufundi na mifumo ya ubunifu kutoka kwa washirika wake.

Katika Jukwaa la Biashara na Uwekezaji la Tanzania–Urusi, Tanzania imeonesha mageuzi yanayolenga kuboresha urahisi wa kufanya biashara. Moja ya kauli zilizosisitizwa zaidi ni kwamba wawekezaji sasa wanaweza kusajili kampuni ndani ya saa 24 ikiwa wana vielelezo vinavyohitajika, ishara ya usasa wa mifumo ya kiutawala na urahisi wa kisheria.

Ujumbe huu uliimarishwa pia katika Mkutano wa Kiuchumi wa Kimataifa wa St. Petersburg (SPIEF), ambapo Rais Samia amewaeleza washiriki kuwa Tanzania ni nchi iliyo wazi na yenye ushindani kwa wawekezaji wa kimataifa. Mkutano huo umewakutanisha viongozi wa dunia, wawekezaji na watunga sera, na kuipa Tanzania nafasi ya kujitangaza katika jukwaa kubwa la uchumi wa dunia.

Matokeo ya moja kwa moja ya ziara hiyo ni mpango wa kuanzisha safari za ndege za moja kwa moja kati ya Dar es Salaam na Moscow zitakazoendeshwa na Air Tanzania kuanzia Julai 2, 2026, pamoja na hatua zinazofanana kutoka kwa shirika la ndege la Urusi.

Hatua hii inatarajiwa kuongeza utalii, kurahisisha safari za kibiashara na kuimarisha uhusiano wa kibiashara kati ya nchi hizo mbili. Safari za moja kwa moja si ishara tu, bali hupunguza gharama za biashara, huongeza imani ya wawekezaji na kuimarisha mahusiano ya watu kwa watu.

Ujumbe muhimu zaidi wa kisiasa uliotokana na ziara hii ni uthibitisho wa Tanzania kuendelea na sera yake ya kutofungamana na upande wowote. Rais Samia amesisitiza kuwa Tanzania inaendelea kushirikiana kwa uwazi na mataifa yote makubwa duniani, yakiwemo Marekani, China, Umoja wa Ulaya, India, Japan na sasa Urusi.

Mtazamo huu unaendeleza misingi iliyoasisiwa na Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere, huku ukibadilishwa kuendana na dunia ya sasa yenye nguvu nyingi za kimataifa (multipolar world). Rais Samia amesema bayana kuwa ziara ya Urusi haikuwa ya kuachana na nchi za Magharibi, bali ya kupanua wigo wa kidiplomasia na kuongeza nafasi ya Tanzania kunufaika na uhusiano na washirika mbalimbali kwa maslahi ya taifa.

Mafanikio ya kweli ya ziara ya Rais Samia nchini Urusi hayaishii kwenye makubaliano yaliyosainiwa au ahadi zilizotolewa, bali katika kasi ya utekelezaji wake. Mchanganyiko wa uwekezaji wa urani, ushirikiano wa nishati ya nyuklia, fursa za elimu, uwekezaji wa miundombinu na uboreshaji wa mawasiliano unaonesha ushirikiano wa muda mrefu wenye uwezo mkubwa.

Hata hivyo, kama ilivyo kwa diplomasia ya ngazi ya juu, kipimo cha mwisho kitakuwa utekelezaji. Ikiwa makubaliano yaliyofikiwa Moscow yatageuka kuwa viwanda vinavyoonekana, ajira kwa vijana, umeme wa uhakika na biashara inayokua, basi ziara hii itakumbukwa kama hatua ya mabadiliko makubwa katika historia ya maendeleo ya Tanzania.

MAWAZIRI WANENA

Waandishi Kulwa Karedia na Aziza Nangwa wanaripoti kutoka Dar es Salaam kuwa, katika hatua nyingine, mawaziri waliombatana na Rais Samia katika ziara hiyo walikutana na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam mwishoni mwa wiki kuelezea mambo mbalimbali ambayo Tanzania itanufaika nayo.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – Mipango na Uwekezaji, Profesa Kitila Mkumbo, amesema Serikali inakwenda kusaka wawekezaji popote walipo duniani bila kuchagua rangi.

“Muktadha wa ziara hii katika mlengo wa uchumi ni utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050. Unahitaji kuhamasisha rasilimali za ndani na nje. Katika kufanya hivyo, sisi kama nchi tutakwenda kusaka wadau popote walipo. Katika hili tutachukua msemo wa wenzetu Wachina kwamba hatutajali rangi ya paka, muhimu awe na uwezo wa kukamata panya.

“Tutaangalia muda, biashara, uwekezaji na teknolojia na kuvifuata popote vilipo. Ndiyo maana tumejipanga vizuri kuhakikisha tunafikia malengo yetu baada ya ziara hii. Tumeunda mikakati yetu. Tulikuwa na vikao tangu mwaka 2024; kikao cha kwanza kilifanyika Dar es Salaam na cha pili Moscow. Katika vikao hivyo vya ushirikiano tumekubaliana kushirikiana katika maeneo takribani tisa,” amesema Profesa Kitila.

Ameyataja maeneo hayo kuwa ni kilimo, elimu na mafunzo, usafiri na usafirishaji, viwanda, utalii, uchumi wa kidijitali na uwekezaji, huku akisisitiza kuwa ushirikiano huo umezaa makubaliano mazuri.

“Mosi, Serikali ya Tanzania na Serikali ya Shirikisho la Urusi zimesaini hati ya makubaliano ya kuendeleza lugha ya Kiswahili na Kirusi. Rais amesema jinsi Kiswahili kinavyofundishwa Urusi, sasa hapa nchini Kirusi kitafundishwa katika Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM). Haya ni matokeo ya kusainiwa kwa makubaliano hayo.

“Hati ya pili ni makubaliano kati ya kampuni ya LDC na Chuo Kikuu cha Afya na Sayansi Shirikishi Muhimbili (MUHAS). Tumesaini mkataba wa kushirikiana katika elimu ya sayansi na teknolojia. Hapa ni muhimu kwa sababu kuna umuhimu wa kutambuliwa kwa tuzo na vyeti vinavyotolewa na vyuo vya Tanzania na Urusi. Zamani ukisoma huko ukirudi nyumbani ulipaswa kupitia mlolongo mrefu wa uthibitishaji. Kikwazo hicho kimeondolewa.

“Mkataba mwingine unahusu ubora na uthibitishaji wa elimu ya Urusi. Watanzania wengi wamesoma huko na sasa suala hilo limetatuliwa,” amesema.

Amesema mkataba mwingine ni kati ya Chuo cha Teknolojia Dar es Salaam (DIT) na taasisi za Urusi.

“Hapa tutakuwa na mpango wa pamoja ambapo vijana wetu watasoma miaka miwili hapa nchini na baadaye kwenda Urusi. Wakirudi watakuwa na shahada mbili,” amesema.

Amesema pia Chuo Kikuu cha Urafiki cha Urusi kitaingia katika ushirikiano wa mafunzo ya akili bandia (AI) na ujifunzaji wa mashine.

“Haya ndiyo maeneo yenyewe kwa sasa duniani,” amesema.

Amesema wameingia pia makubaliano ya kuhamasisha uwekezaji kati ya kampuni ya Urusi na Mamlaka ya Uwekezaji na Kanda Maalumu za Kiuchumi Tanzania (TISEZA).

“Hii ni taasisi kubwa nchini Urusi inayohusika na kuratibu biashara na uwekezaji. Wameingia makubaliano na TISEZA ili kushirikiana katika kuboresha mazingira ya uwekezaji.

“Makubaliano yao makubwa ni kusaidiana kuvutia uwekezaji kutoka Urusi kuja Tanzania, pamoja na kuvutia wawekezaji kutoka nchi nyingine kuja kuwekeza nchini. Pia yatajenga uwezo wa namna ya kuvutia wawekezaji, kuandaa miradi ya ubia kati ya wawekezaji wa Tanzania na wa nje, na kuandaa makongamano ya biashara na uwekezaji yenye hadhi ya kimataifa,” amesema.

Amesema mkataba mwingine ni wa kutunza siri za taarifa kati ya Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) na Kampuni ya ROSATOM.

Tanoni wanataka kuweka miundombinu ya kutengeneza mabehewa na wamekubaliana pia kuanzisha hoteli ya kitalii katika eneo la Ngorongoro ili watalii wafikie.

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Mahmoud Thabit Kombo, amesema Rais Samia ameielekeza UDOM kuanza kufundisha masomo ya Kirusi katika ngazi ya shahada.

Amesema ziara hiyo ni ya kihistoria kwa sababu imeleta mwamko mpya wa ushirikiano katika kipindi ambacho Urusi inajipanga kupanua shughuli zake za kiuchumi katika bara la Afrika, lenye zaidi ya watu bilioni 1.2 na fursa nyingi za uwekezaji.

Mkurugenzi wa Biashara ya Kimataifa na Diplomasia ya Uchumi katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi John Ulanga, amesema safari ya Rais Samia imekuwa na manufaa makubwa, mojawapo ikiwa ni kuanzishwa kwa safari za moja kwa moja za Shirika la Ndege Tanzania (ATCL) kwenda Urusi.

Amesema hatua hiyo itasaidia kuongeza idadi ya watalii, kurahisisha usafiri wa wafanyabiashara na kuimarisha mahusiano ya kiuchumi kati ya Tanzania na Urusi.

Balozi Ulanga amesema Serikali itaendelea kupokea wafanyabiashara kutoka Urusi ambao wameonyesha nia ya kuja kuwekeza nchini baada ya kuona fursa mbalimbali zilizopo.

Amesema ndani ya miezi mitatu ijayo Serikali itatoa taarifa ya utekelezaji wa makubaliano na maelekezo yaliyotokana na ziara ya Rais Samia nchini Urusi.