Na Mwandishi Wetu

Sekta ya Madini imekuwa ni sehemu sahihi ya biashara na uwekezaji kutokana na Miongozo, Maelekezo na Maagizo mbalimbali yanayotolewa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Hayo yameelezwa na Naibu Waziri wa Madini Dkt. Steven Kiruswa akifungua Jukwaa la Madini Tanzania, Sabasaba Expo Village 2023 jijini Dar es Salaam.

Dkt. Kiruswa amesema kuwa, Serikali itaendelea kusaidia na kuweka mazingira bora ya biashara ili kuhakikisha kuwa wawekezaji na wafanyabiashara wanafanikiwa na kuchangia katika ukuaji wa Sekta ya Madini na uchumi wetu.

Amesema, kuanzishwa kwa Jukwaa la 77 Expo Village ni ishara ya dhamira ya kukuza Sekta ya Madini na kuvutia uwekezaji nchini.

“Kupitia jukwaa hili, tunawapa fursa wadau wote walio kwenye mnyororo wa thamani ya madini kuonesha ujuzi na uwezo wao, kutafuta masoko mapya, na kujenga uhusiano na wadau wa ndani na nje ya nchi,” amesema Dkt. Kiruswa.

Kwa upande wake Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Madini Msafiri Mbibo amewashukuru wadau wa Sekta ya Madini kwa kushiriki kikamilifu katika jukwaa hilo la Madini. Amesema Sekta ya Madini itaendelea kutengeneza mazingira rafiki ya biashara na uwekezaji nchini.

Jukwa la Madini Tanzania kimehudhuriwa na Mwenyekiti wa Bodi ya STAMICO Meja General (Mstaafu) Michael Isamuyo, Mkurugenzi Mtendaji wa STAMICO Dkt. Venance Mwasse, Katibu Mtendaji Chemba ya Migodi Benjamini Mchwampaka na wawakilishi kampuni ya Mamba, GGM, Jitegemee Holding, ESAP Mining Service Ltd, Yaya Resources na wadau mbalimbali wa Sekta ya Madini

By Jamhuri