Serikali imeahidi kulipa deni la Sh bilioni 167 la Wakandarasi wazawa pamoja na wa kigeni. Deni hilo limetokana na ujenzi wa miradi mbalimbali katika maeneo tofauti.

Hayo yamesemwa leo na Waziri wa Ujenzi Innocent Bashungwa wakati alipokuwa akizungumza na wakandarasi katika mafunzo ya usimamizi wa mikataba yalioendeshwa na bodi ya usajili wa Wakandarasi(CRB).

Amesema tokea mwezi Agosti mwaka huu, Serikali imeanza kutenga Sh bilioni 70 kwa lengo la kulipa madeni ya wakandarasi ambayo ni Sh bilioni 167.2.

‘’ Katika fedha hizo,Sh bilioni 50 zinalipwa kwa wakandarasi wa ndani na Sh bilioni 20 kwa wakandarasi wageni. Ni mpango wa Serikali kwamba kufikia mwezi Juni 2024, madeni yote yawe yamelipwa.’’ Amesema Bashungwa.

Amewataka wakandarasi kuhakikisha wanafanya kazi zao kwa uweledi na ubora ili kuweza kukamilisha miradi mbali mbali kwa wakati.

‘’Kupitia Taarifa ya Msajili wa CRB, nilibaini kwamba pamoja na kazi nzuri inayofanywa, bado wakandarasi wa ndani ambao ni zaidi ya 96% ya wakandarasi wote waliosajiliwa, mgawanyo wao katika thamani ya miradi haufiki 60%. ‘’ amesema Bashungwa.