Serikali ya Tanzania imesema kuwa imeboresha na kuimarisha mazingira ya kiuwekezaji katika sekta ya mifugo kwa kuondoa baadhi ya ushuru, kodi na vikwazo vya kikodi katika biashara ya mifugo na mazao yake .

Hayo yamelezwa na Waziri wa Mifugo na Uvuvi Abdallah Ulega katika mkutano wake na wadau mbalimbali, kuzinadi fursa zilizopo katika sekta hiyo kando ya Mkutano wa Jukwaa la Mfumo wa Chakula Barani Afrika (AGRF), unaoendelea katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC) leo Septemba 06, 2023.

Waziri Ulega amesema kuwa Tanzania ina idadi kubwa ya mifugo takribani Milioni 77 ikichangia uazilishaji wa tani 80500 za nyama, lita bilioni 3.6 za maziwa, mayai bilioni 5.5 na vipande milion 14.1 vya ngozi kwa mwaka 2023.

“Tanzania imejaliwa kuwa na idadi kubwa ya rasilimali za mifugo takribani milioni 77. Ni shughuli kubwa ya kiuchumi katika angalau kaya milioni 2.2 na inachangia uzalishaji wa kila mwaka wa tani 805,000 za nyama, lita bilioni 3.6 za maziwa, mayai bilioni 5.5, vipande milioni 14.1 vya ngozi na ngozi.” Amesema Ulega

Aidha, Waziri ulega amebainisha kuwa uwepo wa uzalishaji kwa wingi wa mazao ya mifugo kunachangia ulaji wa nyama kila mtu kwa kilo 15, lita 62 za maziwa na Mayai 106 kwa mwakwa ikilinganishwa na viwango vilivyopendekezwa vya Kilo 50, lita 200 na mayai 300 kila mtu kwa kila mwaka.

“Kwa ujumla, mazao ya mifugo yanachangia ulaji wa kila mtu wa kilo 15 za nyama, lita 62 na mayai 106 kwa mwaka dhidi ya viwango vilivyopendekezwa vya Kg 50, lita 200 na mayai 300.”Amesema

Kwa upande mwingine Ulega ameeleza kuongezeka kwa thamani ya mauzo ya nje katika sekta ya mifugo kufikia tani 14.7 za nyama na lita 65,000 za maziwa na kutaja maeneo ya kikanda na kimkakati yapatikanayo Kusini mwa Afrika pamoja na nchi wanchama wa jumuiya ya Afrika mashariki kama soko kubwa la bidhaa za mifugo za Tanzania.

By Jamhuri