SERIKALI imesema Kampeni ya Mtu ni Afya iliyozinduliwa mapema mwezi huu itasaidia udhibiti wa magonjwa yasiyo ya kuambukiza.

Kauli hiyo imetolewa bungeni leo Mei 27, 2024 na Naibu Waziri wa Afya, Dk. Godwin Mollel alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalumu, Shally Raymond aliyehoji Serikali ina mpango gani kuendeleza kampeni ya kunawa mikono, ili kudhibiti magonjwa ambukizi.

Akijibu swali hilo, Naibu Waziri Mollel, amesema serikali imefanya uzinduzi wa kampeni ya Mtu ni Afya kwa awamu ya pili, ambayo inahimiza kuhusu kujengo vyoo bora, lishe bora, udhibiti wa taka, udhibiti wa magonjwa yasiyo ya kuambukiza sambamba na unawaji wa mikono kwa maji na sabuni.

Amesema kampeni hiyo ilizinduliwa Mei 9, 2024 na Makamu wa Rais Dk Philip Mpango na kueleza kuwa, kutekelezwa kwake kutawezesha kudhibiti magonjwa ambukizi katika jamii.