Taasisi ya wanawake na diplomasia yampongeza Rais Samia

Taasisi ya Wanawake na Diplomasia, imetoa pongezi kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk.Samia Suluhu Hassan kwa namna anavyoendelea kutumia diplomasia kuifungua nchini katika nyanja mbalimbali ikiwemo ya uchumi na diplomasia.

Akizungumza leo jijini Dar es Salaam kwenye Kongamano maalum lililoandaliwa na Taasisi ya Wanawake na Diplomasia na kuhusisha mabalozi, wanadiplomasia kutoka taasisi na kampuni mbalimbali, Mwanadiplomasia mkongwe Balozi Liberata Mulamula ametumia nafasi hiyo kuelezea namna ambavyo Rais Samia amekuwa kinara wa diplomasia.

“Diplomasia inatumika katika mambo mengi yakiwemo kuangalia jinsi gani mnaweza kutatua mifarakano, matatizo kwa njia za mazungumzo, kwa njia zuri na huenda wanawake tumezaliwa na huo ujuzi , nimefarikijika kwani mwaka jana taasisi hii ilipotukutanisha kulikuwa na wanawake kutoka Serikalini.

“Wanawake wanaojulikana sana lakini leo tumekuwa na wanawake ambao wametoka kwenye eneo la biashara na tunafahamu hata katika kufanya bashara unatumia diplomasia katika kuvutia biashara yako.Hivyo wakati leo tuaadhimishi siku ya wanawake duniani hawa vijana wameamua tuwe na siku maalumu.

“Kwani huwa tumekuwa tunazungumzia, wanawake katika siasa, wanawake katika biashara lakini leo hii ni wanawake katika diplomasia mimi mnajua ni kama nilizaliwa kwenye diplomasia, nimezeeka kwenye diplomasia lakini hawa vijana wamechukua jukumu la kuhakikisha nchi yetu inaendelea kuzalisha wana diplomasia,”amesema Balozi Mulamula.

Aidha amesema Tanzania kwenye eneo la diplomasia iko vizuri na ndio maana haina nchi adui , hiyo inatokana na kazi kubwa iliyofanywa na Mwalimu Julius Nyerere na sasa chini ya Rais Dk.Samia Suluhu Hassan diplomasia imepaishwa zaidi, amefungua nchi, dunia yote inaangalia Tanzania.

“Ujumbe wangu kwa vijana kwanza mjiamini na mjue inawezekana, jenga mahusiano , ipende kazi unayofanya na muhimu jiheshimu , jiongoze. Kuhusu miaka miwili ya Rais Samia hasa katika nyanja ya Diplomasia kuna mengi ya kusherehekea pengine inahitaji kupindi maalumu.

“Rais amefungua nchi ambayo imetuletea neema , imetuletea faraja katika maeneo yote, diplomasia imepaa , amepanga safu nzuri ya diplomasia kutoka nyanja mbalimbali maana zamani ilikuwa mwana diplomasia lazima atoke Wizara ya Mambo ya Nje lakini yeye amechanganya uzoefu mbalimbali na Tanzania inafika.

“Tunamshukuru sana Rais wetu na leo kwenye jumuiko nilikuwa nawaambia mtu usijifanye sijui nani , kuwa wewe, mnavyomoona Mama Samia ni Mama Samia, tunampenda, tumheshimu, kwa hiyo katika miaka miwili yako mengi na mimi nilipata bahati ya kuhudumu nafasi ya Waziri wa Mambo ya Nje kwa zaidi ya mwaka mmoja na nusu na tarehe 19 anapotimiza miama miwili ya uongozi wake tutakutana pamoja kwa ajili ya kumpongeza.

Kwa upande wake Balozi wa heshima wa Seychell Maryvyonne Poll ambaye amekuwepo nchini Tanzania kwa mwaka wa 41 sasa amesema Rais Samia amekuwa mstari wa mbele kwenye eneo la diplomasia na tangu ameanza kazi ametumia diplomasia katika kutekeleza masuala mbalimbali.

“Diplomasia sio tu lazima kuwa balozi bali wanawake wote ni mabalozi kuanzia nyumbani, katika biashara na ukweli kwa sasa wanawake tunamfuata Mama samia kwasababu yeye ni Mwanadiplomasia namba moja kwa hapa nchini Tanzania,”amesema Balozi Pool.

Kuhusu kongamano lililoandaliwa na Taasisi ya Wanawake na Diplomasia amesema amefurahi kwani amekutana na wasichana wengi na vijana wa Shule ya diplomasia Kurasini, ujumbe wake amewaomba kutokana tamaa ili kufanikisha ndoto yao ya kuwa wana diplomasia na wala wasiogope.

Wakati huo huo Mkurugenzi na Mwanzilishi wa Taasisi ya Wanawake na Diplomasia Kaneni Mushi amesema tukio hilo limewakutanisha mabalozi, wanawake wa taasisi mbalimbali pamoja na vijana wanaosomea diplomasia.Lengo kuu ni kumsherehekea mwanamke katika sekta nzima ya diplomasia lakini kuunga mkono jitihada za Rais Dk.Samia Suluhu Hassan ambaye ndiyo mwanadiplomasia namba moja nchini kwa namna anavyopeperusha bendera anavyofungua uchumi na kulifanya taifa kujulina duniani.

Ametumia nafasi hiyo kueleza taasisi hiyo imejikita katika uchumi wa diplomasia , hivyo wanashukuru wadau wengi kujitokeza huku akieleza kufunguliwa kwa milango ya diplomasia nchini wanashuhudia maendeleo yanavyoongezeka.

“Tanzania tunatambulika,tunaheshimika , tunaona vijana wengi wanafanya vitu vikubwa, wana kampuni zao, wana taasisi zao, hivyo tunamshukuru Rais Dk.Samia Suluhu Hassan kwa jinsi ambavyo amefungua diplomasia ya uchumi.” amesema.