Na Shamimu Nyaki,JamhuriMedia

Timu ya Taifa ya Wanawake chini ya Miaka 17 ( Serengeti Girls), inatarajia kucheza na Colombia katika robo fainali baada ya kuandika historia kwa mara kwanza kufuzu hatua ya Robo Fainali ya Kombe la Dunia baada ya kuitoa timu ya nchini Canada.

Mechi ya Robo Fainali baina ya Tanzania ( Serengeti Girls) na Colombia itachezwa Oktoba 22, jijini Goa India.

Katika mchezo na Canada,Serengeti Girls ilikua inahitaji kushinda sare ya aina yoyote,katika mechi hatimaye ilifanikiwa kupata sare ya goli 1 – 1.

Naibu Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo Mhe. Pauline Gekul ameongoza Watanzania kuishangilia na kutoa hamasa ya kutosha kwa timu hiyo, ambapo amesema Tanzania sasa inatangazwa vyema kupitia Sekta ya michezo.

Akizungumza mara baada ya mchezo kumalizika, Gekul ameishukuru Serikali chini ya Rais Samia Suluhu Hassan kwa kuwezesha timu hiyo ya Serengeti kuanzia kuweka Kambi ya kutosha katika Mji wa Southampton nchini Uingereza ambapo ilifanya maandalizi mazuri ambayo yameifikisha hapo timu hiyo.

“Nawapongeza sana wanangu hawa, wameliheshimisha Taifa, wameitangaza Tanzania, sasa hivi sio Royal Tour peke ake inayoweza kuitangaza nchi yetu bali hata Sekta ya michezo imeiweka Tanzania kuwa miongoni mwa nchi zenye vipaji na kujulikana zaidi” amesema Gekul.

Kwa upande wa Kocha Bakari Shime,amesema Wasichana wamefanya vizuri baada ya kufuata maelekezo aliyowapatia pamoja na kurekenisha makosa waliyoyaona katika mechi zao mbili za kwanza, huku akisema Wasichana hao siku zote wana ari ya ushindi na wamekua na utulivu kiakili pamoja na nidhamu ya hali ya juu.

Tanzania Sasa inaungana na Japan katika kundi D kutinga hatua ya robo fainali, baada ya kuifunga Ufaransa na kutoa sare na Canada na hatimaye kupata alama nne nyuma ya Japan wenye alama 9.

By Jamhuri