Na David John , Jamhurimedia, Kigoma

Shirika la Uwakala wa Meli Tanzania (TASAC) limekutana na wadau mbalimbali mkoani Kigoma na kukusanya maoni juu ya maombi ya mapitio ya tozo yaliyowasilishwa na Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA) uliofanyika Juni 30,2023 mkoani Kigoma.

Akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu Deogratias Mukasa (TASAC), amesema ilipokea maombi ya mapitio ya tozo za huduma za Bandari zinazotolewa katika bahari kuu ya Dar es salaam na maziwa kutoka Mamlaka ya Usimamizi Wa Bandari Tanzania (TPA) kwa lengo la kuhuisha tozo ili kuendana na mazingira ya biashara ya sasa katika bandari za bahari na maziwa.

“Ni wajibu wa Shirika kupokea maombi ya tozo na kukusanya maoni ya wadau ili kusaidia kutathmini maombi yaliyowasilishwa na kubaini ukweli wa hali ya soko mchakato huu ni matakwa ya kifungu cha 29 cha Sheria ya Uwakala wa Meli Tanzania Sura 415 na wadau wanaweza kutoa maoni yao” amesema Bw. Deogratias.

Aidha ameongeza kuwa mikutano hii inatoa fursa kwa TPA na wadau kutoa maoni kwa uhuru na uwazi kwa kupendekeza viwango vya tozo rafiki kabla ya TASAC kupitia na kuchakata ili kufanya maamuzi kuhusu maombi yaliyowasilishwa.

Mukasa ametoa wito kwa wadau kuendelea kutoa maoni kupitia ofisi za TASAC zilizopo mkoani Kigoma au kupitia barua pepe ([email protected] hadi tarehe 20 Julai, 2023..

Zoei la kupokea maoni limefanyika katika Mkoa wa Dar es Salaam, Mtwara, Mwanza na Kigoma.

By Jamhuri