Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendelea ya Makazi, Jerry Slaa amewataka watumishi wa ardhi nchini, kuwa waadilifu na hofu ya Mungu kwa kutenda haki wakati wanaposuluhisha migogoro ya ardhi.

Slaa ameyasema hayo mapema leo Aprili 15, 2024, wakati akifungua kliniki ya ardhi Mkoa wa Mbeya itakayofanyika hadi Aprili 17, 2024, Jijini hapa. Amewakumbusha watumishi wa Ardhi kutenda haki kwa wananchi na kuwa na hofu ya Mungu, kwani kushindwa kutatua jambo ambalo lipo ndani ya uwezo wao ni kumkosea Mungu.

Aidha Slaa ameendelea kusisitiza kufanya kazi kwa kumsaidia Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan lakini pia kufanya kazi kwa ajili ya wananchi katika upande wa ardhi ili kupunguza kero na migogoro isiyokuwa na ulazima katika jamii.

Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Mbeya Mhe. Juma Homera amempongeza Mhe. Slaa kwa kuitumikia vyema sekta ya ardhi kwa kutatua migogoro mbalimbali nchini ikiwa ni moja ya jitihada za kumsaidia Rais kwa vitendo.

Katika Kliniki hiyo ya Ardhi inayofanyika katika ukumbi wa Mkapa, wakazi wa Mkoa wa Mbeya watapata huduma ya kusikilizwa na kutatuliwa changamoto mbalimbali zinazohusu ardhi.

By Jamhuri