Wakulima Manyara walia upatikanaji ruzuku ya mbolea

Wakulima mkoani Manyara wameiomba Serikali kuangalia namna ya kusambaza mbolea ya ruzuku kutokana na usumbufu wanaoupata kwa kukosekana vituo vya karibu.

Wakizungumza na kituo cha redio cha Smile FM, baadhi ya wakulima kutoka Dareda, Mamire na maeneo mengine ya wilaya ya Babati wanasema wanatumia gharama kubwa kwa ajili ya usafiri kufuata Mbolea Mjini Babati huku wakieleza kwao hawaoni unafuu licha ya ruzuku iliyotangazwa na Serikali.

Changamoto nyingine waliyoitaja wakulima hao ni kupata namba ya malipo kwa wakati pamoja na mfumo wa kutambua orodha ya walioandikishwa kusuasua ilihali msimu wa kilimo umefika.

Ofisa Kilimo Mkoa wa Manyara Paulina Joseph, alikiri changamoto hiyo kujitokeza kwa wakulima na kuahidi wataangalia namna ya kuongeza mawakala maeneo ya karibu na kueleza kuwa tayari wameweka mawakala wilaya ya Babati, Hanang’, Mbulu,Kiteto na Simanjiro.

Amesema pembejeo zingine kama mbegu zipo karibu kila eneo changamoto ni kwenye mbolea pekee hivyo wakulima waifuate mbolea hiyo inapopatikana ili wasipitwe na msimu wa kilimo wakati serikali inatafuta utatuzi.

Amesema serikali imeamua kuwaandikisha wakulima wote na kuwapatia ruzuku ya mbolea kwa bei nafuu ya shilingi 70,000 kutoka bei ya zamani 150,000 ili mkulima alime kwa tija na kuwa na uhakika wa chakula.