Takriban wanajeshi 320 wa Sudan walitoroka mapigano yanayoendelea nchini Mwao hadi nchi jirani ya Chad, waziri wa ulinzi wa Chad alisema Jumatano.

Waziri wa ulinzi Jenerali Daoud Yaya Brahim aliuambia mkutano wa waandishi wa habari kwamba “Waliwasili kwenye ardhi yetu, walipokonywa silaha na kuwekwa kizuizini siku ya Jumapili.”

Alisema wanajeshi wao wamehofia kuuawa na wanamgambo wa kikosi cha Rapid Support Forces ( RSF) kinachopambana na wanajeshi wa mkuu wa jeshi na kiongozi wa Baraza kuu la Sudan Jenerali Abdel Fattaf al-Burhan.

Waziri huyo amesema “Hali nchini Sudan inatia wasiwasi na inasikitisha, tumechukua hatua zote zinazohitajika ili kukabiliana na mzozo huu.”

Ameongeza hata hivyo kwamba “vita hivi havituhusu, ni vita kati ya Wasudan, na lazima tuwe waangalifu dhidi ya matukio yote.”

Amejizuia kutoa maelezo zaidi, katika siku ya tano ya mapigano mjini Khartoum na kwingineko nchini Sudan, ambayo yamesababisha vifo vya raia wasiopungua 270, kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na balozi za kigeni Jumatano.

Jumamosi, Chad ilifunga mipaka yake na Sudan, yenye urefu wa zaidi ya kilomita 1,000 katika jangwa, ambayo mara nyingi huvukwa na makundi ya waasi kutoka nchi zote mbili.

By Jamhuri