Watu wanne walipatikana Alhamisi wakiwa wamefariki na wengine zaidi ya kumi wamelazwa hospitalini katika kaunti ya pwani ya Kilifi nchini Kenya, baada ya kuokolewa wakisubiri ‘mwisho wa dunia unaokaribia’.

Polisi walisema kundi hilo lilipatikana katika msitu walimokuwa wakiishi kwa siku kadhaa baada ya kuambiwa na mhubiri wa eneo hilo kufunga huku “wakingoja kukutana na Yesu”.

Mamlaka ilisema iliokoa watu 11 – sita kati yao walikuwa wamedhoofika na katika hali mbaya ya afya.

Polisi walisema wataanza tena msako wa kuwatafuta wanachama zaidi wa kundi hilo Ijumaa asubuhi kufuatia ripoti kwamba wengine walikuwa bado msituni.

Polisi wanaripotiwa kupata kaburi msituni ambalo litachunguzwa siku ya Ijumaa.

Waumini hao ni wa Kanisa la Good News International Church linaloongozwa na mchungaji wa eneo hilo ambaye amekuwa akiangaziwa na polisi kwa madai ya kuwataka waumini wake kufa njaa ili kufika mbinguni kwa kasi.

Kwa sasa mhubiri huyo yuko huru baada ya kuachiliwa kwa dhamana ya polisi baada ya kushtakiwa mwezi uliopita kuhusu kifo cha watoto wawili ambao wazazi wao ni miongoni mwa wafuasi wake.

By Jamhuri