Na Mwandishi Wetu

Waziri wa Ujenzi, Innocent Bashungwa ametoa wito kwa wapangaji wote kuhakikisha kuwa wanalipa kodi za pango kwa wakati ili kuepusha usumbufu kwao na kwa Wakala wa MajengoTanzania (TBA).

Waziri Bashungwa aliyasema hayo juzi Bungeni Jijini Dodoma wakati akiwasilisha Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa fedha ujao 2024/25.

Bashungwa alisema katika mwaka wa fedha 2023/24 TBA iliingia na deni lenye jumla ya Shilingi bilioni 14.35 ambapo kutokana na jitihada kubwa zilizofanywa na Wizara kupitia huo katika kipindi tajwa, TBA imefanikiwa kukusanya jumla ya Shilingi bilioni 4.3.

“Hii ni sawa na asilimia 30 ya malimbikizo ya deni, hivyo, deni lililobaki ni Shilingi bilioni 10.05”,alisema.

Aidha aliongeza kuwa TBA inaendelea na jitihada za kufuatilia ulipaji wa madeni hayo kwa kutumia dalali wa mahakama ili fedha hizo zitumike kukarabati nyumba zilizopo, na kujenga nyumba mpya ili kukidhi mahitaji yaliyopo.