Ahadi hiyo imetolewa na Rais wa Umoja wa Watayarishaji wa Filamu wa Korea (Korean Films Producers Association-KFPA), Bw. Eun Lee mbele ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan alipokutana nao jijini Seoul Juni 01, 2024.

Wakati wa kikao hicho ambacho kilihudhuriwa na wasanii maarufu nchini Tanzania, Mhe. Rais Samia alieleza kuwa Tanzania ina wasanii wengi wenye vipaji isipokuwa wanakosa ujuzi, vifaa na miundombinu ya kutayarishia filamu zinazokidhi viwango vya kimataifa, hivyo, aliwaomba Wakorea ambao filamu zao zinatayarishwa na kuigizwa kwa viwango vya hali ya juu washirikiane na wenzao kutoka Tanzania.

Rais Samia alimwambia Bw. Eun kuwa filamu za Korea zinapendwa na kuangaliwa na watu wengi nchini Tanzania, hivyo, alishauri waangalie uwezekano wa kutumia maeneo mazuri na ya kuvutia yanayopatikana nchini Tanzania kutayarisha na kuigiza filamu zao.
‘Tanzania tuna mito, misitu, maziwa, mbuga za wanyama na utamaduni wa aina tofauti ambao unafaa kwa kuigizia filamu na kufanya kuwa na mvuto wa hali ya juu duniani”, Rais Samia alisema.


Rais Samia aliwashauri wapange mapema ziara ya kutembelea Tanzania ili kuangalia maeneo hayo na kwamba ziara yao ya kwanza, Serikali yake itagharamia.
Wasanii hao akiwemo Lulu Michael, Monalisa, Ramata walimshukuru Rais Samia kwa kuwapaginia changamoto wanazokabiliana nazo ambazo ni pamoja na ujuzi, vifaa na miundombinu ya kutayarishia filamu.


Walisema Rais Samia ni mpenzi wa filamu na kiasharia kuwa yeye ni mpenzi wa filamu ni uamuzi wake wa kucheza filamu mbili ambayo moja ya filamu hizo ni filamu maarufu duniani ya Tanzania The Royal Tour.


Ushirikiano wa Tanzania na Korea katika sekta ya filamu utakuwa ukombozi kwa wasanii wengi wa Tanzania. Korea ina utaalamu na miuondombinu ya hali ya juu ya kutayarisha filamu na sekta ya filamu katika nchi hiyo inaingizia Serikali pesa nyingi kila mwaka. Inakadiriwa kuwa Korea inaingiza Dola za Marekani milioni 600 kutokana na mauzo ya filamu nje ya nchi.