Na Mwandishi Wetu, JamhuriMedia, Dodoma

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu nayeshugulika na Sera, Bunge na Uratibu Jenista Mhagama, Amepokea Rasimu ya kwanza ya Mwongozo wa Kitaifa wa Ufuatiliaji na Tathmini ya Utendaji wa Shughuli za Serikali katika Taasisi za Umma.

Akipokea Rasimu hiyo, tarehe 24/08/2023 Jijini Dodoma, Waziri Mhagama alisema Mwongozo wa Kitaifa wa Ufuatiliaji na Tathmini ya Utendaji wa Shughuli za Serikali Nchini, Utasaidia kuwa na matokeo ambayo yanaendana na programu na Miradi iliyopangwa kutekelezeka ndani ya Taifa, na Itasaidia Serikali kujipangia Programu zenye matokeo chanya.

“Tunaweza tukawa na matokeo yakawa hasi, ama mradi usifanye vizuri, ila tukiwa na Mwongozo mzuri basi utatusaidia ndani ta Taifa kuwa na matokeo mazuri yaliyowekwa kutokana na Utekelezaji wa mradi Husika” alibainisha.

Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu) Mhe. Jenista Mhagama akizungumza baada ya kupokea taarifa kuhusu maandalizi ya Rasimu ya mwongozo wa Kitaifa wa Ufuatiliaji na Tathimini katika Taasisi za Umma kikao kilichofanyika katika Ukumbi wa Ofisi hiyo Jijini Dodoma

Sambamba na hilo, alisema kuwa, mwongozo huu utafikisha Taifa mahali ambapo dhana ya uwajibikaji wa hiari na uratibu wa Pamoja itafikiwa na kujifanyia tathmini katika usimamizi na utekelezaji wa programu, zilizopo nchini na Usimamizi mzuri wa Rasilimali watu na Rasilimali fedha kwenye Serikali kuu, Taasisi na Serikali za Mitaa.

Aidha, Mhe. Waziri Mhagama Alisema ana Imani kuwa Muongozo huu, utasaidia kuimarisha Utawala Bora na kuendelea kusema kuwa, bila Utawala bora hakuna kizuri kitakachofanyika, katika dhana nzima ya kutelekeza kazi za kila siku akitolea mfano dhana ya uwajibikaji na mapambano dhidi ya rushwa.

“Tunatarajia kuwa Mwongozo huu Utatusaidia kutekeleza Dira ya Taifa ya Maendeleo, Ilani ya Uchaguzi ya Chama Tawala na Mpango wa Maendeleo wa Muda Mrefu na muda Mfupi.” Alihimiza.

Naibu Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu) Bw. Anderson Mutatembwa akifuatilia kikao cha kupokea taarifa kuhusu maandalizi ya Rasimu ya mwongozo wa Kitaifa wa Ufuatiliaji na Tathimini katika Taasisi za umma kilichofanyika katika Ukumbi wa Ofisi hiyo Jijini Dodoma.

Aliongeza kusema kuwa Mwongozo huu utasaidia kukamilisha programu na miradi Pamoja na kufikisha huduma kwa wananchi kwa wakati na viwango vinavyotarajiwa na kuokoa Rasilimali fedha kwa kiasi kikubwa.

“Nauona huu Mwongozo ni kitu cha Muhimu na kipekee,Tunataraji mwongozo huu utusaidie ndani ya Serikali kupanga miradi na program zetu kwa kuzingatia vipaombele tulivyonavyo, kwenye Sekta, Taasisi, Mashirika ya Umma na wakala lakini hata kwenye Sekta Binafsi sababu wale ni washiriki wetu kimaendeleo.” Alifafanua

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Kikosi Kazi cha kuandaa Mwongozo wa Kitaifa wa Ufuatiliaji na Tathmini ya Utendaji wa Shughuli za Serikali Dkt. Fransis Mwaijande, alisema Uandaaji wa Mwongozo huo umetokana na kuiwezesha Ofisi ya Waziri Mkuu kutekeleza jukumu la Kikatiba ambapo limeainishwa katika Katiba ya Jamhuri ya Muungango wa Tanzania Ibara ya 52 fungu cha 1-3 ya mwaka 1977, mbayo inaipa Ofisi ya Waziri Mkuu Mamlaka ya Kusimamia Shughuli za Serikali ikiwemo Ufuatiliaji na Tathmini wa Sera Mipango, Miradi na Programu za Maendeleo na Utendaji wa Shughuli za Serikali kwa Ujumla.

Awali, Akiongea wakati wa wasilisho la Mwongozo huo, Mkurugenzi wa Idara ya Ufuatiliaji na Tathmini kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, bunge na Uratibu Bi. Sakina Mwinyimkuu alisema, rasimu hiyo ya Mwongozo wa Ufuatiliaji na Tathmini ni miongoni mwa document ambayo itatumika wakati wa kongamano la pili la Kitaifa Ufuatiliaji na Tathmini litakalofanyika Mwezi Septemba Mkoani Arusha.

Baadhi ya Wakurugenzi wa Idara na Wakuu wa Vitengo Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu) pamoja na kikosi kazi wakifuatilia kikao cha kupokea taarifa kuhusu maandalizi ya Rasimu ya mwongozo wa Kitaifa wa Ufuatiliaji na Tathimini katika Taasisi za umma kilichofanyika katika Ukumbi wa Ofisi hiyo Jijini Dodoma.

By Jamhuri