Na Mwandishi Wetu, JamhuriMedia

Kfuatia maelekezo ya Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Kassim Majaliwa Majaliwa ya kumsimamisha kazi Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Uvinza mkoani Kigoma Zainab Mbunda na Mwekahazina wa Halmashauri hiyo Majid Mabanga, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa Mohamed Mchengerwa (Mb) amemwelekeza Katibu Mkuu Ofisi ya Rais – TAMISEMI kutekeleza maelekezo ya Waziri Mkuu mara moja kwa kuwasimamisha kazi Mkurugenzi na Mwekahazina huyo kuanzia leo tarehe 21, 9, 2023 ili kupisha uchunguzi.


Uamuzi huo umefikiwa mkoani Kigoma mara baada ya Waziri Mkuu Mhe. Majaliwa kukagua ujenzi wa hospitali ya Wilaya na Jengo la Halmashauri ambayo licha ya Mkurugenzi kukiri kuwepo kwa fedha za utekelezaji wake tangu mwaka 2021 ujenzi wake bado haujakamilika.


Aidha Waziri Mchengerwa amemuelekeza Katibu Mkuu Ofisi ya Rais -TAMISEMI kuteua afisa atakayekaimu nafasi ya Mkurugenzi na Mwekahazina hadi hapo uchunguzi utakapokamilika.


Vilevile Mchengerwa amewataka Wakurugenzi wote wa Mamlaka za Serikali za Mitaa kusimamia utekelezaji wa miradi ya maendeleo kwenye maeneo yao kwa kuzingatia thamani ya fedha na kuhakikisha inakamilika kwa wakati huku wakihakikisha ukusanyaji wa mapato ya ndani ya halmashauri unafanyika kikamilifu ili kupeleka maendeleo kwa wananchi
Pia amesisitiza kuwa hatua za nidhamu zitachukuliwa kwa Watendaji watakaoshindwa kutekeleza majukumu yao kikamilifu na kusababisha ucheleweshwaji wa upatikanaji wa huduma bora kwa wananchi.

By Jamhuri