Waziri wa Katiba na Sheria, Prof Palamagamba Kabudi amekosoa utaratibu uliotumiwa na Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda katika kushughulikia tatizo la wanawake wanaodai kutelekezwa na wazazi wenzao.

Waziri Kabudi ameyasema hayo jana bungeni baada ya Mbunge wa Viti Maluum (CHADEMA), Sabrina Sungura kumtaka waziri huyo kueleza kwanini Mkuu wa Mkoa anavunja sheria mbalimbali za nchi.

Sabrina alimtaka Waziri Kabudi ambaye jana bunge lilikuwa likijadili bajeti yake kuwa, atakapokuja kujibu hoja za wabunge kuhusu hotuba ya bajeti yake aeleze sababu za kiongozi huyo wa mkoa kukiuka sheria za nchi.

Akizungumza katika mjadala huo jana Aprili 18 bungeni, Sabrina amesema moja ya sera zinazovunjwa na mkuu huyo wa mkoa ni pamoja na kuvunja mabaraza ya ardhi ya kata yaliyopo kisheria.

“Huyu mkuu wa mkoa, hivi sasa amesababisha hata hayo mabaraza hayafanyi kazi, ni kwanini anavunja sheria namna hii?” Amehoji Sungura.

By Jamhuri