Na Mwandishi Wetu, JamhuriMedia, Dodoma

Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Jerry Silaa amesema zoezi la urasimishaji linaloendelea maeneo mbalimbali nchini litaboreshwa ili kuleta ufanisi.

Silaa amesema hayo tarehe 21 Mei 2024 wakati wa semina kwa Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi Maliasili na Utalii kuhusu Utekelezaji Mradi Uboreshaji Usalama wa Milki za Ardhi nchini (LTIP) hadi kufikia Mei 15, 2024 iliyofanyika kwenye ukumbi wa Samwel Sitta Bungeni jijini Dodoma.

Amesema, maboresho hayo ya zoezi la urasimishaji yatawafanya wananchi kuelewa kuwa, kuishi eneo rasmi kama vile lile la mita za mraba 750 kuna faida zaidi ukilinganisha na kuishi eneo lenye ukubwa wa mita za mraba 1000 lisilo rasmi.

‘’Wananchi waelewe kuishi eneo rasmi lenye square mita 750 kuna faida ukilinganisha na kuishi eneo la square mita 1000 lisilo rasmi’’ Amesema.

Amewataka wananchi wanaorasimishiwa maeneo yao kutekeleza dhana ya kujitolea wakati wa zoezi hilo kwa kuwa, ndiyo dhana ya ujamaa na falsafa ya Tanzania inayomfanya mwananchi kuelewa sehemu ya eneo lake imetolewa kwa ajili ya matumizi ya huduma kama vile barabara, makaburi na shule.

Amebainisha kuwa, utekelezaji huo ukifanyika basi uvamizi kwenye maeneo ya wazi unaofanyika sasa kwenye maeneo mbalimbali utapungua.

‘’Tunapopanga na kupima maeneo, mtu anapopata kiwanja chake basi ajue nina kiwanja eneo fulani lakini kuna maeneo ya umma ambayo yapo na wakati mimi napata kiwanja nimeyalipia’’ amesema Mhe. Silaa,

Kwa mujibu Mhe. Silaa, yapo maelekezo kwa maeneo yanapopangwa na kupimwa kwamba mtu anaponunua kiwanja chake cha makazi ajue hawezi kuishi peke yake na atakuwa amelipia pia maeneo ya huduma kama vile ya kuabudia na kuzikia.

Kwa upande wake Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Geophrey Pinda amewaeleza wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi Maliasili na Utalii kuwa, Wizara yake imeendelea kutoa elimu hususan kwenye maeneo yanayomilikishwa kwa hati.

Ametolea mfano wa uwekaji mipango ya matumizi ya ardhi katika vijiji kuwa, zoezi hilo limekuwa likihusisha wananchi wa maeneo husika huku akiweka wazi kuwa, elimu imekuwa ikitolewa kwa makundi mbalimbali ili kujua umuhimu na namna ya kutunza hati.

‘’Ushirikishwaji katika zoezi mipango ya matumizi ya ardhi kwenye vijiji ni mkumbwa sana maana wanaokwenda kusimama na zoezi ni wananchi wenyewe kwa hiyo utoaji elimu ni mkubwa na wananchi wanaelimishwa kwa makundi ili kuelewa hati inayokwenda kutolewa’’ amesema.

Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi imeendesha semina ya siku moja kwa wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Ardhi Maliasili na Utalii kwa lengo la kuelezea hatua zilizofikiwa kwenye Mradi wa Uboreshaji Usalama wa Milki za Ardhi Tanzania (LTIP) hadi kufikia Mei 15, 2024.

Mradi huo unatekelezwa kupitia vipengele vinne ambavyo ni kuongeza usalama wa milki za ardhi, kuimarisha mifumo ya taarifa za ardhi (ILMIS), kujenga miundombinu ya ardhi pamoja na kusimamia mradi.

By Jamhuri