Na Mwandishi Wetu, JamhuriMedia,Dodoma

Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora George Simbachawene amewapongeza Idara ya Elimu sekondari ya Halmashauri ya wilaya ya Mpwapwa kwa kufanya vizuri katika Mtihani wa kidato cha nne kwa kushika nafasi ya kwanza kimkoa na kushika nafasi ya pili kimkoa kwa matokeo ya kidato cha pili.

Kauli hiyo ameitoa wakati alipokutana na Ujumbe huo bungeni leo tarehe 07/02/2024 jijini Dodoma, Ujumbe uliongozwa na Mwenyekiti wa Halmashauri ya wilaya ya Mpwapwa George Fuime na Afisa elimu Sekondari pamoja na Maafisa elimu na walimu wakuu wa sekondari 32 za Halmashauri ya wilaya ya Mpwapwa.

Amesema kila jambo linalotokea lina msingi wake, na Msingi Mkuu ni utendaji mzuri wa ushirikiano katika kazi kwa kuangalia mazuri ya kila kitu na mazuri ya kila mtu.
“Kuangalia mazuri ya wanafunzi mazuri ya walimu, na mazuri ya viongozi yanasaidia katika kuweza kupata matokeo mazuri,” alisema Waziri.

Mwenyekiti wa Halmashauri ya wilaya ya Mpwapwa Mhe. George Fuime (kushoto) akiwa na Maafisa Elimu na Walimu kutoka Halmashauri ya wilaya ya Mpwapwa waakifuatilia kikao cha Bunge, wakati wa Bunge la 12 Mkutano wa 14 unaoendelea jijini Dodoma.

Kwa upande wake Afisa elimu sekondari Halmashauri ya wilaya ya Mpwapwa Mwalimu Bernadetha Thomas amesema Waziri amewaalika baada ya kufanya vizuri matokeo ya kidato cha nne.

“Tumepanda kutoka asilimia 88 kiwango cha mwaka juzi mpaka 95 kwa wanafunzi waliopata ufaulu wa daraja la kwanza mpaka daraja la nne kwa mwaka 2023 na mchango huu umechangiwa na shule kumi na moja za kata alisema,” Afisa elimu sekondar.

Tumechukua ushauri wa Mhe Waziri kama maelekezo kwetu kwa kuwa amekuwa akituongoza katika mabadiliko chanya katika sekta ya elimu

Waziri wa Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. George Simbachawene akiwa katika picha ya pamoja na Mwenyekiti wa Halmashauri ya wilaya ya Mpwapwa Mhe. George Fuime (Kulia) na Maafisa elimu na Walimu wa sekondari Halmashauri ya wilaya ya Mpwapwa.